September 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Dkt.Tulia avitaka vikundi vya ngoma vilivyoshinda kubadilisha maisha yao

Na Esther Macha,TimesmajiraOnline,Mbeya

VIKIUNDI vya ngoma za asili vilivyoshiriki Tamasha la Tulia Traditional Dance Festival 2024,Jijini Mbeya na kupata zawadi za ushindi vimetakiwa kwenda kuboresha maisha kutoka hatua moja kwenda nyingine kujikwamua kiuchumi.

Imeelezwa katika washindi wa tamasha la msimu wa nane wapo ambao wamefanya vizuri tangu Taasisi ya Tulia Trust ianzishe mashindano hayo.

Kauli hiyo imetolewa jana Septemba 28,2024 na Spika wa Bunge,Mbunge wa Jimbo la Mbeya na Rais Umoja wa Mabunge Duniani,(IPU) Dkt.Tulia Ackson wakati akifunga mashindano ya ngoma za asili yaliyofanyika katika uwanja wa ndege wa zamani katika kata ya Iyela Jijini hapa.

Dkt.Tulia amesema lengo la Tamasha hilo ni kuhakikisha utamaduni unaenziwa kupitia chakula na ngoma na kutumia fursa hiyo kama kitega uchumi na ushiriki wa ubalozi wa China kutoa zawadi.

“Niombe vikundi vyote vitakavyoshinda zawadi wakaboreshe maisha na kutumia vizuri na kubadilika kimaisha kupitia uchezaji ngoma na vyakula vya asili “amesema.

Ameongeza kuwa “,Niwaombe nyie mnaocheza ngoma mjitahidi kuwarithisha wanaowafuata nyuma kama ambavyo mlivyorithishwa na wazazi wenu ili tutakapo ondoka miaka 100 ijayo wale wanaobaki wawe wameachiwa maadili mema na utamaduni tuliorithi kwa wale waliotutangulia,”amesema Dkt.Tulia.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Machifu Tanzania,Antonia Sangalali amesema kuwa Dkt.Tulia ni dhahabu inayotembea aheshimiwe na apendwe kwani ni jeshi kubwa na mama.

“Dkt.Tulia ni jeshi kubwa ,machifu wanakupenda iwe mvua ,jua sisi na Dkt.Tulia ni mama na mwana,tunamshukuru Rais Samia ni jeshi kubwa tupo nyuma yake yawe mafuriko mvua,jua,yawe matope tupo kwa ajili yenu sisi machifu “amesema Chifu Sangalali.

Akizungumza katika Tamasha hilo Mstahiki Meya wa Jiji la Mbeya,Dourmohamed Issa ambaye ni Diwani kata ya Isanga amesema kwamba tamasha mwitikio huo mkubwa kwa wananchi unaonyesha kuwa wanamkubali Rais Samia pamoja na Dkt.Samia.

“Katika mkoa wa Mbeya Tamasha hili ni msimu wa Nane na kwa Jiji la Mbeya ni mara ya Nne kwa mkusanyiko huu mkubwa wa watu kwani umeleta fursa za kibiashara kwa wananchi ambapo kupitia Tamasha hilo la ngoma kumeleta tija kubwa ya biashara kwa wajasiriamali wa nje ya Mbeya na hapa “amesema Meya Issa.

Mashindano ya ngoma za asili yamehitinishwa jana ambapo zaidi ya vikundi 150 ambao ni sawa na 3700 kutoka mikoa mbalimbali hapa nchini vilishiriki mashindano hayo na vikundi vilivyoshinda vilipatiwa za piki piki na wengine fedha.