May 17, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Dkt.Kikwete azifagilia JKT Queens,JKT Tanzania

Na Joyce Kasiki,Timesmajira online,Dodoma

RAIS Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.Jakaya Kikwete ameipongeza Timu ya soka ya wanawake  JKT Queens kwa kufanya vizuri katika mashindano mbalimbali huku akilitaka Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) kutafuta walimu wazuri wa kufundisha timu zake.

Aidha Dkt.Kikwete ameipongeza timu ya JKT Tanzania kwa kufanya vizuri na kuingia katika msimu ujao wa Ligi Kuu Tanzania Bara .

Rais Mstaafu Dkt.Kikwete ametoa pongezi hizo wakati akizungumza kwenye mashindano ya mbio za JKT (JKT Marathon)  ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya miaka 60 ya JKT tangu kuanzishwa kwake huku akiitaka JKT kupambana kuhakikisha timu hiyo inafanya vizuri katika msimu ujao wa Ligi Kuu Bara .

“Mwaka huu JKT Queens wamefanikiwa kutwaa ubingwa wa ligi Kuu wanawake ,ni mafanikio makubwa sana ukizingatia kwamba wamepata ubingwa kwa kuipokonya timu mashuhuri timu ya Simba Queens ,naipongeza sana,

“Pia naipongeza  Timu ya JKT Queens kwa kushiriki  michezo ya Majeshi Duniani yanayofanyika nchini Uholanzi ,wameshinda lakini mafanikio yanategemea pia kupata walimu wazuri,wekezeni mpate walimu  wazuri wa kufundisha hii .”amesema Dkt.Kikwete

Kiongozi huyo ametoa rai kwa JKT kuhakikisha wanaendeleza  jitihada za kubuni na kuanzisha mashindano ya riadha na michezo mingine ili kuendeleza kukuza vipaji vingi zaidi na kwamba hatua hiyo itasaidia kuwawezesha vijana hapa nchini kukabiliana na changamoto za ajira lakini pia kujenga afya zao.

Pia amelitaka Jeshi hilo kufikiria suala la kuanzisha kituo cha michezo (Academy) ambacho kitafundisha vijana wadogo kwa ajili  kuwafundisha na kukuza vipaji kwa vijana hapa nchini.

Kwa upande wake Mkuu wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania Jenerali Jacob MKunda amesema,Jeshi hilo linapenda michezo na limekuwa likiibua vipaji vya watu ambao wameenda kushinda hadi nje ya nchi na kurudisha heshima hapa nchini.