October 6, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Dkt. Kikwete awataka wahitimu UDSM kuwa mabalozi wazuri

Na Jackline Martin, TimesMajira Online

Mkuu wa Chuo kikuu cha Dar es Salaam, (UDSM) Rais Mstaafu wa awamu ya nne Daktari. Jakaya Mrisho Kikwete amewataka wahitimu wote wa chuo hicho kuwa mabalozi wazuri ndani na nje ya Tanzania kwa kukitangaza vyema chuo chao.

Dkt. Kikwete ameyasema hayo
katika Mahafali ya 54 ya chuo kikuu cha Dar es Salaam yaliyofanyika leo Oktoba 5, 2024 katika ukumbi wa Mlimani City Jijini Dar es Salaam ambapo amewapongeza wahitimu hao kwa kufikia hatu hiyo.

“Nawapongeza wahitimu wote kwa kufikia hatua hii, mnapotoka hapa nendeni mkawe mabalozi wazuri wa chuo kikuu cha Dar es Salaam” Amesema Dkt. Kikwete

Kwa upande wake Makamu Mkuu wa
Chuo kikuu cha Dar es Salaam, Profesa William Anangisye amewasihi wahitimu wa chuoni hapo mbali na kusuburi ajira za serikalini , wawe wepesi kuangalia fursa nyingine kwa kutumia maarifa na ujuzi walioupata masomoni.

Pia awamewataka wahitimu hao kupeleka thamani yao kwa jamii ya Tanzania, Afrika na Duniani kote kwa kuonesha utofauti kwa kutoa ufumbuzi wa changamoto zinazoikabili jamii.

“Tambueni kuwa elimu imeongeza thamani yenu, nina maana kuwa mlivyo leo sivyo mlivyokuwa miaka mitatu, minne au mitano iliyopita , thamani yenu imepanda sana, nawaomba mpeleke thamani yenu kwa jamii ya Tanzania, Afrika na Duniani , ni wakati wenu kwenda kuonesha tofauti , sio wakati wa kulaumu bali kutoa ufumbuzi wa changamoto zinazoikabili jamii”

Aidha Prof. Anangisye amewasihi wahitimu hao kutumia elimu waliyoipata kuleta faida kwa watanzania kama Mwalimu Julius Kambarage Nyerere alivyosema “Tunatumia fedha nyingi sana zisizolingana na uwezo wetu kuwasomesha watu wachache, ili baadaye na wao walete faida kubwa kiasi hicho hicho katika nchi”

Kutokana na hivyo, Prof. Anangisye amewasihi wadau ikiwa ni pamoja na wazazi kuiunga mkono serikali katika kuwekeza katika elimu ya watoto wa kitanzania.

Pia Prof. Anangisye amewataka wahitimu hao ambao wanaorudi ofisini wakumbuke kuzingatia sheria, taratibu , kanuni na miongozo ya utumishi ya umma katika kuwatumikia watanzania

Kadhalika, Prof. Anangisye amewataka wahitimu hao kuzingatia maadili ya jamii ya kitanzania na kiafrika kwa ujumla

“Ya ulaya waachie wa Ulaya” Amesisitiza Prof. Anangisye

Prof. Anangisye amewasihi wahitimu hao kutumia ujana wao kwa faida.

“Watanzania wanatarajia mengi kutoka kwenu, hakuna mtu asiyetambua mchango wa vijana wanaojitambua katika kuendeleza Taifa.”

Mbali na hayo, Prof. Anangisye alimshukuru Mkuu wa Chuo hiko, Rais Mstaafu wa awamu wa nne Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete , Balaza la Chuo na wadau wote kwa ushauri na miongozo ambayo mahafali hayo ni moja ya matunda yake.

Pia ameishukuru serikali na wadau kwa kuendelea kutoa rasilimali zinazohitajika katika kuendesha shughuli za chuo ikiwemo jukumu la kuwafunza wahitimu wa mwaka huu kwa viwango vinavyostahiki.

Naye Mwenyekiti wa Baraza la Chuo kikuu cha Dar es Salaam, Balozi Balozi Mwanaidi Maajar amewasihi wahitimu hao kuwa na busara katika kuzikabili changamoto za maisha watakazokumbana nazo huku akiwataka kuongeza bidii kutafuta fursa halali za kuendeleza maisha.