May 3, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Dkt.Jingu azindua mradi wa mzunguko wa saba wa kutokomeza Ukimwi, kifua kikuu na Malaria

Na Zena Mohamed,Timesmajiraonline,Dodoma

Katibu Mkuu Wizara ya Afya,Dkt.John Jingu amezindua mradi wa mzunguko wa saba wa Mfuko wa Dunia (Global Fund Circle7)ambao utatekelezwa kwa muda wa miaka mitatu kuanzia sasa kwajili ya kutokomeza Ukimwi,Kifua kikuu na Malaria nchini Tanzania ili kutokomeza Magonjwa hayo ifikapo Mwaka 2030.

Amesema serikali imepokea jumla ya dola za kimarekani milioni 602 sawa na trilioni 1.4 za kitanzania kwa ajili ya kukabiliana na magonjwa ya Malaria, Kifua Kikuu na Ukimwi katika kipindi cha miaka mitatu kuanzia mwaka 2024 hadi 2026.

Dkt.Jingu amezindua mradi huo,leo Machi 21,2024 Jijini hapa, ambapo amewataka wanaotekeleza Mradi huo kufanya kazi kwa ufanisi ili kuongeza tija katika kutokomeza magonjwa hayo.

Amesema kuwa fedha zilizopokelewa zimetokana na jitihada za Serikali ya awamu ya sita chini ya uongozi wa Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan katika kuboresha huduma za afya ili ziweze kuwafikia wananchi katika maeneo yao bila kikwazo.

“Ni muhimu sana sisi ambayo tunatekeleza Mradi huu kuhakikisha tunatumia fedha ambazo tumefadhiliwa na Mfuko huu wa Dunia kwa malengo yaliyokusudiwa kwa Wananchi,”amesema Dkt. Jingu

Amefafanua kuwa Serikali ya awamu ya sita ya Rais Dkt.Samia imekuwa ikiwekeza fedha nyingi katika Sekta ya afya kwa lengo la kuboresha afya za Wananchi wake na Kuwataka watumishi hao kufanya kazi zao kwa weledi mkubwa.

Kwa upande wake,Mganga Mkuu wa Serikali,Profesa Tumaini Nagu amesema wapo kwaajili yakujipima na kuangalia walipotoka na walipo ili kufika malengo ya Kidunia namba tatu kwa kutekeleza Strategic Plan ya afya namba tano.

“Serikali imeona umuhimu katika kutokomeza magonjwa haya ambayo ni Ukimwi,Kifua Kikuu na Malaria ili kuhakikisha inatokomeza magonjwa haya ifikapo Mwaka 20230,”amesema Prof.Nagu

Awali Mwakilishi wa Serikali ya Marekani ambao Pia wanatekeleza Mradi wa PEPFAR,Etruda Temba amesema wanatambua mchango wa Tanzania katika mapambano dhidi ya Magonjwa hayo huku akiwasisitiza kufanya kazi kwa umakini katika kuhakikisha rasilimali wanazopatiwa wanazitumia kwa usahihi.