Na Esther Macha, Timesmajira Online, Mbeya
Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati,Dkt. Dotto Biteko, ameonesha kufurahishwa na mwitikio wa wananchi wa Mbeya katika mashindano ya Riadha ya Betika Tulia Marathoni, ambayo mwaka huu ni msimu wa tisa.
Akizungumza Mei 10, 2025, jijini Mbeya wakati wa kufunga mashindano hayo, Dkt. Biteko amesema mwaka huu idadi ya washiriki imefikia 2,000 kutoka 1,760 mwaka 2024, ikiwa ni ongezeko la asilimia 13, jambo linaloashiria hamasa kubwa ya wananchi.

“Mwamko huu ni uthibitisho wa upendo mlionao kwa Dkt. Tulia, na ni njia nzuri ya kuimarisha afya zenu,”amesema Dkt.Biteko.
Aidha,amevutiwa na ubunifu wa Dkt. Tulia,ambapo amesema kuwa amekuwa kiunganishi kwa wananchi na wajasiriamali kupitia mWarathon hiyo.
“Ukitazama leo, wafanyabiashara wanafaidika, amewaweka pamoja, amewaunganisha. Wewe ni mwalimu wa wengi. Nakupongeza kwa ubunifu huu,” amesema Dkt. Biteko.
Kwa upande wake, Spika wa Bunge na Mbunge wa Mbeya Mjini, Dkt. Tulia Ackson,amesema mashindano hayo yamelenga kuchochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi, hasa kwenye sekta ya afya na elimu. Mapato kutoka kwa mashindano huwekezwa kwenye miundombinu ya sekta hizo.

Amosi Juma, mkazi wa Ilomba jijini Mbeya, alieleza kuwa mashindano hayo yameleta fursa kwa wajasiriamali.
“Mashindano haya yanatufaa sana sisi wafanyabiashara. Tunatamani yafanyike kwa siku tano kwani yameinua vipato vyetu,” amesema Juma.
More Stories
Miaka 50 ya TET, waanza kupanda miti
Mwili wa Hayati Msuya wawasili Uwanja wa Ndege wa (KIA)
Mapato yasiyo ya kodi yafikia asilimia 67, OMH yadhamiria kufikia lengo la mwaka