July 5, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga Debora Magiligimba

BREAKING NEWS: AKAMATWA KWA KUSAMBAZA TAARIFA ZA UONGO KUHUSU CORONA

Na Suleiman Abeid, Shinyanga

JESHI la Polisi mkoani Shinyanga linamshikilia mwanafunzi wa mwaka wa tatu katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kitivo cha Kiswahili kwa kosa la kusambaza kwenye mitandao ya kijamii taarifa za uongo kuhusu ugonjwa wa Corona.

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Shinyanga, Debora Magiligimba amemtaja mwanafunzi aliyekamatwa kuwa ni, Mariamu Jumanne Sanane (23) ambaye alikamatwa Aprili 9, mwaka huu saa 02.07 usiku eneo la mtaa wa Tabora katika Mgodi wa Almasi wa Mwadui wilayani Kishapu mkoani Shinyanga.

Kamanda Magiligimba alisema, mnamo Machi 26, mwaka huu askari wa Kikosi kazi cha mitandao ya kijamii walifanikiwa kuona ujumbe kwenye mtandao wa whatsap uliotumwa na mtuhumiwa ukisomeka,
“…Mpk ss Tanzania ina wagonjwa wapatao takriban 230 wa COVID 19 na waliofariki ni 04.”

Mtuhumiwa baada ya kupekuliwa alikutwa na simu iliyotumika kutuma ujumbe huo ambapo tayari amehojiwa na anatarajiwa kufikishwa mahakamani kwa makosa ya kuchapisha na kusambaza taarifa za uongo mitandao ni na kutoa takwimu za uongo.

“Naomba nitoe wito kwa wananchi wote kuwa makini na matumizi ya mitandao ya kijamii na waache kupotosha watu waweze kufanya hivyo ni kosa la jinsi watachukuliwa hatua Kali za kisheria,” alisisitiza Kamanda Magiligimba.