April 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Brazil na Tanzania zasaini Mkataba Mradi wa Kilimo cha Pamba wenye lengo la kuimarisha utafiti,kuongeza thamani

Na Zena Mohamed,Timesmajiraonline,Dodoma.

SERIKALI ya Tanzania na  Brazil zimesaini mkataba wa mradi wa utafiti wa mbegu ya pamba,usalama wa chakula na masuala ya lishe (BEYONDCOTTONPROJECT)wenye gharama ya Dola za Marekani 930,118 wenye lengo kuimarisa utafiti pamoja na kuongeza Thamani ya zao la pamba hapa nchini.

Ambapo Nchi ya Brazil pekee itachangia Dola za Marekani 629,700,Bodi ya Pamba Tanzania (TCB) ikichangia dola za kimarekani 289,022 huku shirikisho la chuo kikuu Campina Grande(UFCG) wakichangia dola za Marekani 11,396 .

Wakisaini Mkataba huo jijini hapa leo  Balozi wa Brazil Nchini Tanzania,Antonio Cesan,Mkurugenzi wa Shirika la Chakula  Duniani (WFP),Gunga Mbavu pamoja na Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya pamba Marco Mtunga ambaye pia ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo amesema kuwa mradi huo wa utanufaisha kaya Zaidi ya 8400 wenye  dhumuni la kuimarisha tija katika uzalishaji wa zao la pamba.

Mtunga amesema kuwa kwa pamoja wanatambua kuwa  kilimo bora cha pamba kitaimarisha uchumi wa watanzania na wakulima kwa ujumla.

“Mkataba wa kilimo bora cha pamba ni kuendeleza thamani  ya pamba na utafiti wa mbegu bora zisizoshambuliwa na wadudu na magonjwa kama ilivyokuwa hapo awali,”amesema.

Ameeleza kuwa kwa sasa miti ya pamba haitachomwa moto na badala yake zitakuwepo kwa ajili ya kuchakata miti hiyo na kuigeuza kuni pamoja na mashine za kusokota nyuzi jambo ambalo litaongeza tija katika kilimo cha pamba.

Kwa upande wake Balozi wa Brazili Nchini Tanzania,Antonio Cesan amesema kuwa Brazil wataendelea kushirikiana na nchi ya Tanzania kwa kuimarisha kilimo cha Pamba nchini ili kuwa na tija katika zao hilo.

“Matarajio yetu wakulima wapatao kaya 8400 watanufaika katika mradi huu wakiwemo vijana kwa asilimia 50,wanawake kwa asilimia 30 na wanaume asilimia 20 na mradi huu utatekelezwa katika mkoa wa mwanza katika Wilaya ya Magu, Misungwi na Kwimba lengo ni kuongeza kipato kwa wakulima wadogo wadogo,

“Tumepanga ifikapo mwaka 2030 kilimo kikue kwa asilimia 10,na mradi huu umelenga agenda za kilimo tulizo jiwekea ambazo ni kuongeza tija katika uzalishaji wa pamba na thamani yake pamoja ambapo mradi huo ukikamilika unatarajiwa kufanikisha malengo sita ya maendeleo endelevu,”amesema Cesan.

Ametaja malengo hayo kuwa ni lengo namba moja ni kupunguza umasikini,namba mbili kupunguza njaa,lengo namba tano kuleta usawa wa kijinsia,lengo namba tisa ukuzaji viwanda na miundombinu,lengo namba 12 uwajibikaji katika matumizi na uzalishaji na lengo namba 17 kuleta masuala mtambuka katika kuleta ushirikiano katika kufanikisha malengo yote.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Utafiti wa Mbegu TARI,Geofrey Mkamilo amesema kuwa Taasisi hiyo itaendelea kufanya utafiti wa mbegu bora ambazo zitaongeza tija kwa wakulima wapamba.