October 6, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Squad ya Aston Villa ambayo imefanya yake kuinusuru timu yao kushuka daraja. (Picha na Aston Villa FC).

Aston Villa ya kina Samatta yanusurika kushuka daraja, Liverpool mabingwa

Na Mwandishi Wetu, TimesMajira Online, London

Hatimaye Ligi Kuu ya England imemalizika leo baada ya michezo ya raundi ya 38 kuchezwa ambapo Klabu ya Liverpool wamekuwa mabingwa wa ligi hiyo kwa jumla ya alama 99, huku Aston Villa ikinusurika kushuka daraja.

Mtanzania Mbwana Ally Samatta amekuwa sehemu ya kikosi cha Aston Villa, ambaye ameiwezesha kuinusuru kushuka daraja baada ya sare ya 1-1 na wenyeji West Ham United katika uwanja wa London.

Kwa mujibu wa mashabiki wa Aston Villa kutoka nchini Tanzania waliozungumza na TimesMajira Online wamesema kuwa,kunusurika kwa Villa kutokushuka daraja kumewapa faraja kubwa, kwani wanaamini bado Samatta ataendelea kuwawakilisha.

Jack Grealish alianza kuifungia Aston Villa dakika ya 84 akimalizia pasi ya kiungo mwenzake, Mscotland John McGinn bao lililodhaniwa litakuwa la ushindi.

Aidha, mshambuliaji, Andriy Yarmolenko baadae aliisawazishia West Ham United dakika ya 85 akimalizia pasi ya kiungo wa England, Declan Rice.

Kwa matokeo hayo, Aston Villa inakamilisha msimu wa Ligi Kuu ya England na pointi 35, ikizizidi pointi moja moja AFC Bournemouth na Watford zilizoungana na Norwich City kushuka daraja.

Mbali na hayo, baada ya Liverpool na Man City kujihakishia kucheza ligi ya mabingwa barani ulaya msimu ujao mapema,Man United na Chelsea nao wamejikatia tiketi ya kushiriki michuano hiyo mikubwa ya Ulaya.

Man United wakiwa ugenini katika dimba la King Power wamewafunga wenyeji wao Leicester City kwa magoli 2-0 kwa magoli ya Bruno Fernandes kwa mkwaju wa penati na Jesse Lingard na hivyo kumaliza ligi katika nafasi ya tatu.

Huu ndiyo mtiririko wa matokeo ya michezo yote ya leo katika Ligi Kuu ya England, Arsenal 3 – 2Watford, Burnley 1 – 2 Brighton & Hove Albion, Chelsea2 – 0Wolverhampton Wanderers,Crystal Palace 1 – 1 Tottenham Hotspur,Everton 1 – 3 AFC Bournemouth, Leicester City 0 – 2 Manchester United, Manchester City 5 – 0 Norwich City,
Newcastle United1 – 3 Liverpool,Southampton 3 – 1 Sheffield United na West Ham United 1 – 1 Aston Villa.