July 7, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

AGRA mwenyeji mkutano wa sera wa vijana,ubadilishaji wa mifumo ya chakula

Na Mwandishi wetu, Timesmajira

TAASISI inayojitolea kuweka Wakulima Wadogo katika Kitovu cha Uchumi Barani Afrika (AGRA)inatarajia kuwa mwenyeji wa Mkutano wa Sera wa Vijana na Ubadilishaji wa Mifumo ya Chakula,utakaowakutanisha  wawakilishi wa vijana, washirika wa utekelezaji  na wadau muhimu katika mlolongo wa thamani ya mifumo ya chakula.

Mkutano huo unalengo la kuwakutanisha wadau hao na kufanya mazungumzo na vijana ili kuelewa mahitaji yao na vipaumbele vyao vizuri zaidi na kujadili mambo mbalimbali ikiwemo  hatua za sera muhimu za kuwawezesha vijana katika kilimo, kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi, na kuhakikisha mabadiliko katika mifumo ya chakula.

Akizungumza katika hafla ya mkutano na waandishi wa Habari katika jiji la Dar es Salaam, Mkurugenzi wa Nchi wa AGRA, Vianey Rweyendela amesema  kupitia mkutano huo matokeo makubwa yanayotazamwa kama ramani ya njia ya kujenga mazingira yanayosaidia ujasiriamali, fursa za soko zinazolingana, uzalishaji wa kilimo wenye ushindani, ujumuishaji wa kifedha ulioboreshwa, nafasi za vijana katika utawala, na kuimarisha taasisi za kusaidia vijana.

Amesema matokeo yanayotarajiwa ya Mkutano huoni mapendekezo ya sera,maendeleo ya muhtasari wa sera wenye tija ili kuunga mkono ushiriki wa vijana katika mifumo ya chakula inayostahimili mabadiliko ya hali ya hewa na hati ya kumbukumbu ya michango ya vijana katika kuimarisha na kukuza programu zinazolenga vijana.

”Mada mbalimbali zitakazojadiliwa zitahusu upatikanaji wa ardhi,upatikanaji wa fedha, huduma za maendeleo ya biashara, utetezi wa sera na kukabiliana na mabadiliko ya hali ya hewa,”amesema Rweyendela 

Akizungumza kwa niaba ya Katibu Mkuu katika Wizara ya Kilimo, Gerald Mweli, Kiongozi wa Programu ya Kujenga Kesho Bora kutoka Wizara ya Kilimo, Vumilia Zikankuba amesema kuwa wizara ina lengo la kutoa mwongozo wa sera na huduma kwa mfumo wa kilimo na ushirika ulioimarishwa, uliokomeshwa kibiashara, wenye ushindani na wenye ufanisi.

Ameipongeza  AGRA kwa kazi yake ya kubadilisha sekta ya kilimo nchini Tanzania na kusema kuwa juhudi zake zinaendana na malengo na mipango ya maendeleo ya serikali.

”Serikali ya Tanzania inajitahidi kutoa huduma za kilimo na ushirika zenye ubora, kutoa mazingira mazuri kwa wadau,kuimarisha uwezo wa Mamlaka za Serikali za Mitaa na kuwezesha sekta binafsi kuchangia kwa ufanisi katika uzalishaji endelevu wa kilimo, tija na maendeleo ya ushirika,”amesema Zikankuba.

Mkutano huo unatarajiwa kuhudhuriwa na Waziri wa Kilimo,  Hussein Mohamed Bashe,pamoja na wwadau mbalimbali wa masuala ya Kilimo ndani na nje ya nchi.