May 12, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

ACT Wazalendo yajipanga kuimarisha ushiriki wa wanawake kwenye uongozi.

Na Mwandishi wetu,Online

KATIBU Mkuu wa ACT Wazalendo, Ado Shaibu amesema Chama hicho kimejipanga kuongeza ushiriki wa wanawake kwenye nafasi mbalimbali za uongozi za ndani ya Chama na kwenye chaguzi za Kiserikali kuanzia Uchaguzi wa Serikali za Mitaa wa 2024 na Uchaguzi Mkuu 2025.

Katibu Mkuu ameyasema hayo kwenye Mikutano Mikutano ya ACT Wazalendo katika Majimbo ya Pangani na Mkinga iliyofanyika Juni 26 na 27,2023.

“Jana nilikuwa Pangani na leo nipo hapa Mkinga. Kwenye Mikutano Mikuu hii nimefarijika sana na ushiriki mkubwa wa viongozi wanawake kutokea katika Kata ambao ndio wajumbe wa Mkutano Mkuu. Hali hii inatia moyo sana kwa sababu ukombozi wa kweli wa jamii yetu kisiasa, kiuchumi na kijamii utapatikana iwapo wanawake watashirikishwa ipasavyo”,amesema na kuongeza

“Hata hivyo, hatupaswi kuishia katika ngazi ya Kata pekee. Ni lazima wanawake wajitokeze kwa wingi zaidi kugombea kwenye ngazi za jimbo, mkoa na Taifa. Wanawake pia jipangeni kushiriki kwa wingi kwenye uchaguzi ujao wa Serikali za Mitaa na Uchaguzi Mkuu kwenye nafasi mbalimbali,”amesema Katibu Mkuu.

Katibu Mkuu amesema Chama kimejipanga kuwajengea uwezo wa kiuongozi viongozi wanawake katika ngazi za majimbo ili waweze kushiriki ipasavyo kwenye chaguzi za Serikali za Mitaa 2024 na Uchaguzi Mkuu 2025.

Jana tarehe 27 Juni, Katibu Mkuu wa ACT Wazalendo Ndugu Ado Shaibu amehitimisha ziara yake ya siku tatu Mkoani Tanga ambapo ametembelea majimbo ya Tanga Mjini, Pangani na Mkinga. Kwenye ziara hiyo, Katibu Mkuu amekutana na viongozi wa Kata 63 za majimbo hayo kupitia mikutano mikuu ya majimbo.