April 26, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

ACCT wampongeza Rais Samia kutwaa tuzo ya Babacar Nchini Ghana

Na Zena Mohamed,Timesmajiraonline,Dodoma.

CHAMA cha Wakandarasi Wazawa (ACCT) kimesema Rais Samia Suluhu Hassan alistahiri kupewa tuzo ya heshima ya Babacar aliyoipata Mei 25 mwaka huu katika mkutano mkuu wa mwaka wa Benki ya maendeleo ya Afrika(AfDB),Accra nchini Ghana, kwasababu amefanya mambo makubwa katika sekta ya miundombinu ikiwemo ujenzi wa reli ya kisasa, barabara na bandari.

Kutoka na Tuzo hiyo Chama hicho kimeandaa kongamano maalumu la wakandarasi Wazawa kwa ajili ya kumpongeza Rais Samia kwa kutwaa tuzo  hiyo na kuifanya Tanzania kutambulika Kimataifa.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini hapa leo kuhusu kongamano lililoandaliwa na wakandarasi wazawa kwajili ya kumpongeza Rais Mwenyekiti wa ACCT Thobias Kyando amesema ujenzi wa miundombinu umekuwa na faida hasa kwa wandarasi Wazawa kwasababu wao ndiyo wanaohusika moja kwa moja kuiboresha pindi wakandarasi wageni wanapoondoka.

Mwenyekiti huyo pia alitumia fursa hiyo kuiomba serikali kuendelea kuwaamini wakandarasi wazawa kwa kuwapatia tenda mbalimbali ili waendelee kupata uzoefu hiyo itasaidia kuipunguzia serikali gharama ambazo imekuwa ikitumia kutoa tenda kwa kampuni za nje ya nchi.

“Ni vyema wakandarasi wazawa wakawa wanahusika moja kwa moja katika kutekeleza miradi mbalimbali inayotekelezwa hapa nchini kwani hiyo  itasaidia serikali kutumia fedha kidogo na kupata uzoefu kutoka kwa wakandarasi wa kigeni,”amesema.

Kwa upande wake makamu mwenyekiti wa ACCT  Profesa Mhandisi John Bula amesema wamendaa kongamano kubwa litakalofanyika katika ukumbi wa Jakaya kikwete Dodoma lengo ni kutoa pongezi kwa Rais Samia kwa kutwaa tuzo hiyo ya heshima.

Pia amemtaja Waziri wa ujenzi na uchukuzi Makame Mbarawa kuwa mgeni rasmi katika kongamano hilo.

“Kesho tutatoapongezi kubwa kwa Rais wetu kwa kupata  tuzo kubwa ambayo inatupa nguvu kwasababu hata sisi wakandarasi wazawa ameendelea kutujali kwa kutupatia kazi mbimbali za ujenzi  tunachoomba tupewe fursa zaidi ili tuonyeshe uwezo zaidi kwasababu utaalamu unaweza ukanunuliwa kutoka nje kwa pale tutakapokwama,”amesema

Naye Mwanachama wa ACCT Maida Waziri ameeleza kuwa tuzo aliyoipata Rais Samia ni tuzo kubwa watanzania hawana budi kuendelea kutambua na kuunga mkono jitihada mbalimbali zinazofanywa na serikali katika sekta ya miundombinu.

Amesema kupitia tuzo hiyo Dunia imeweza kumtambua hivyo kama watanzania lazima kutambua umuhimu wa kile alichopewa Rais Samia na kutembe kifua mbele kwasababu haikuwa kazi rahisi kuchukua tuzo hiyo.

“Tuzo hiyo ameipata kutokana na ujenzi wa miundombinu kwa kweli tuna haki ya kujivunia sana kwa sababu kama watanzania Rais Samia ameleta tuzo hiyo kubwa napenda kusema kuwa watanzania  tunaona dira na muelekeo wa serikali ya awamu ya sita tunaona njia kubwa huko tunakoenda,”amesema

Maida amesema kigezo cha nchi kuonekana ni tajiri mara nyingi hupimwa kwenye ujenzi wa miundombinu na kwa tuzo hiyo ambayo Rais Samia ameipata ameonyesha watanzania  kuwa Tanzania ni  nchi  tajiri.

“Rais Samia amepewa tuzo na Benki ya Afrika imetambua jitihada anazozifanya katika ujenzi wa miundombinu ya barabara ikiwemo miradi aliyoikuta iliyoanzishwa na  hayati Dk.John magufuli na kuanzisha miradi mipya,”amesema.