March 8, 2026

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Bulugu azungumza na bodaboda Mbozi awasisitiza kumpa kura za kishindo Dkt.Samia

Na Mwandishi wetu,Timesmajira


Katibu Msaidizi Mkuu Idara ya Uhamasishaji na Chipukizi wa CCM, Bulugu Magege ameambatana na katibu Uhamasishaji na Chipukizi Mkoa wa Mbozi leo na kukutana na vijana bodaboda wa Wilaya ya Mbozi na kuwasisitiza kuhakikisha kura zao zote zinakwenda kwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, wabunge na madiwani wa CCM.

Bulugu amewakumbusha vijana kuwa Dkt. Samia anawapenda na kuwajali vijana na mara kwa mara amekuwa akitoa fursa nyingi kwa vijana mfano ni mikopo ya asilimia 10 kupitia Halmashauri kwa vikundi vya vijana, wanawake na wenyeulemevu.

Amesema hata kundi la bodaboda ni miongoni mwa walengwa wakuu wa fursa hizo, ili waweze kujitegemea kiuchumi na kukuza kipato chao.

Kwa upande wao, vijana bodaboda wa Mbozi walimhakikishia Bulugu kuwa wanaimani kubwa na Dkt.Samia kwani kafanya maendeleo mengi Mkoa wa mbozi huduma za afya, Barabara,  miradi ya elimu  hivyo 29 oktoba watampa kura za kishindo.


Wakati huo huo amezungumza na  wafanyakazi wa Kiwanda cha Mbozi Coffee Curing na kuwasisitiza wajibu wao wa kizalendo wa kumpa kura za kishindo Dkt. Samia Suluhu Hassan, pamoja na wagombea wa CCM katika nafasi za Ubunge na Udiwani.

Katika mazungumzo hayo, Bulugu amewaeleza kuwa Dkt. Samia ni Kiongozi mwenye upendo na watanzania anayejali wakulima na wafanyakazi kwa kuendeleza sekta ya kilimo na viwanda hususani kahawa, ambayo ni uti wa mgongo wa wananchi wa Mbozi na mkoa mzima wa Songwe.

Amesisitiza kuwa kura zao kwa Dkt. Samia ni kura za maendeleo ya kweli kwa taifa

Katika ziara hiyo, Bulugu aliambatana na  Haji Shabani Mwalimu, Katibu wa UVCCM Wilaya ya Mbozi na Noel Donald Mkwemba, Katibu wa Uhamasishaji na Chipukizi Mkoa wa Songwe wote kwa pamoja wamewaeleza wafanyakazi hao kuwa CCM ni chombo pekee cha kuwaletea mustakabali bora na kuwataka watimize ahadi yao ya kumpa ushindi wa kishindo Dkt. Samia ifikapo Oktoba 29, 2025.