March 7, 2026

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Regina Lubala aahidi kuwezesha wanawake wa Pasiansi kupitia mikopo 

*Ni endapo atachaguliwa  kuwa Diwani Pasiansi

*Kukutana na wanawake na kuwapa elimu sahihi ya mikopo na matumizi yake

Na Judith Ferdinand, Timesmajira Online-Mwanza 

Mgombea Udiwani wa Kata ya Pasiansi, Jimbo la Ilemela mkoani Mwanza kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM),Regina Lubala, ameahidi kuwasaidia wanawake wa kata hiyo kunufaika na mikopo ili kujikwamua kiuchumi na kuondokana na changamoto zinazowakabili kwa sasa.

Akizungumza  na Timesmajira Online,Lubala amesema endapo atapata ridhaa ya kuwa Diwani katika uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba 29, 2025, atahakikisha wanawake wanapewa kipaumbele katika kupata elimu ya mikopo na matumizi sahihi ya fedha hizo.

“Ni yangu ya kugombea  nafasi hii ni kuleta maendeleo kwa wananchi wa Pasiansi.Wanawake wengi hawana maendeleo si kwa sababu hawana uwezo  bali kukosa elimu ya namna ya kupata mikopo na kutumia fedha hizo kwa ajili ya kuanzisha biashara,”amesema Regina. 

Lubala ameeleza  kuwa mikopo ya kuwainua wanawake ipo, lakini changamoto  ni ukosefu wa uelewa wa jinsi ya kuifikia na kuitumia kwa tija.

Pia amesisitiza kuwa baadhi ya wanawake wamekuwa wakichukua mikopo lakini huishia kuitumia kwa matumizi yasiyo ya maendeleo, jambo linalowaacha katika hali ileile ya umasikini.

“Nitakapochaguliwa kuwa Diwani nitawapa kipaumbele wanawake  wa Kata hii,kwanza kwa kukutana nao na kuwapa elimu juu ya upatikanaji wa mikopo,mahali pa kuipata na jinsi ya kuitumia ili iwasaidie kuinua maisha yao na familia zao.Hili ndio nitakalolipa kipaumbele namba moja,”amesema Regina.

Sanjari na hayo,Lubala ametumia nafasi hiyo kuwaomba wananchi wa  Kata ya Pasiansi kumpa kura ili aweze kutimiza azma yake ya kuwawezesha wanawake na kuleta maendeleo katika kata hiyo kwa ujumla.

0-4064×3074-0-0#