Na Agnes Alcardo,Timesmajira Online
MKURUGENZI Mkuu wa Mamlaka ya Udhibiti Mkondo wa Juu wa Petroli (PURA), Charles Sangweni, amesema kuwa sekta ya gesi asilia na sekta ya kilimo ni sekta zinazotegemeana kwa karibu na kwamba sekta hizi zikifungamanishwa vizuri zitaongeza tija katika uchumi.
Sangweni ameyasema hayo leo Agosti 07, 2025 alipotembelea Maonesho ya Kimataifa ya Kilimo ya Nane Nane yanayoendelea Jijini Dodoma.
Sangweni alibainisha kuwa, gesi asilia inayozalishwa nchini inaweza kutumika kama malighali kuzalisha ammonia, kemikali ambayo hutumika kuzalisha mbolea za aina mbalimbali ikiwemo urea.

Pia ameongeza kuwa, matumizi ya gesi asilia kwenye magari yamesaidia kupunguza gharama za uendeshaji hivyo gesi asilia ikitumiwa katika magari yanayosafirisha mazao ya kilimo, mifugo na uvuvi itasaidia kupunguza gharama za usafirishaji.
Kwa upande mwingine, Sangweni ameeleza kuwa sekta ya kilimo imeendelea kuwa nguzo muhimu katika utekelezaji wa miradi ya mafuta na gesi asilia kwa kulisha wataalamu wanaofanya kazi katika miradi ya mafuta na gesi asilia nchini.
Pamoja na sekta ya kilimo kutoa huduma hii muhimu, Sangweni alisema bado kumekuwa na changamoto kadhaa ikiwemo kampuni hususan kampuni za nishati za kimataifa kuhitaji bidhaa za kilimo zenye ubora na viwango ambavyo watoa huduma wachache wakitanzania wanakidhi.
Hata hivyo, Sangweni amebainisha kuwa, PURA kwa kushirikiana na wadau mbalimbali imeendelea kufanya jitihada za makusudi kuhakikisha kuwa viwango na ubora hitajika vinafikiwa kwa maslahi mapana ya uchumi.




More Stories
TAMWA yakumbusha jamii kupinga ukatili wa kijinsia kuelekea siku ta wanawake Duniani
Wanawake washauriwa kuchangamkia fursa za uchumi
Aida:Wanawake wakipata haki zote itapunguza migogoro