March 7, 2026

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Ushirikiano wa Wizara ya Katiba na Sheria na Mambo ya Ndani ya Nchi  Wapongezwa,wananchi wakaribishwa kupata msaada wa kisheria

Na Joyce Kasiki, Timesmajira online,Dodoma

Naibu Katibu Mkuu kutoka Wizara ya Mambo ya Ndani  ya Nchi Maduhu Kaziamepongeza ushirikiano kati ya wizara hiyo na Wizara ya Katiba na Sheria  katika kushughulikia masuala mbalimbali yakiwemo ya haki jinai nchini.

Akizungumza katika banda la Wizara ya Katiba na Sheria kwenye Maonyesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea jijini Dodoma, kiongozi huyo amesema Wizara ya Katiba na Sheria ni muhimili muhimu katika kuimarisha mifumo ya utoaji haki, hivyo inapaswa kushirikiana kwa karibu na vyombo vyote vya ulinzi na usalama ili kufanikisha haki kwa wote.

Ameomba ushirikiano huo uendelee   ili kwa pamoja waweze kuhakikisha kwamba masuala ya hakijinai yanafanyiwa kazi kwa utaratibu ambao unatakiwa.

“Nafurahi kuona ushirikiano huu unajengwa kuanzia ngazi ya watendaji wa Wizara hizi mbili na siyo Mawaziri peke yao,hatua hii inaendelea kuimarisha masuala ya utoaji haki katika maeneo mbalimbali likiwemo la hakijinai nchini.”amesema Naibu Katibu Mkuu huyo

Naibu Katibu Mkuu huyo ametumia nafasi hiyo kuwaasa wananchi wa mkoa wa Dodoma na mikoa jirani kujitokeza kwa wingi kwenye banda hilo ili kupata huduma za kisheria kwa maslahi yao na Taifa kwa ujumla.

Awali Wakili wa Serikali Wizara ya Katiba na Sheria Nickson Maleko amesema, katika maadhimisho hayo, wizara hiyo imejipanga kutoa huduma za msaada wa kisheria kwa wananchi na watumishi wenye uhitaji wa msaada wa kisheria.

Amesema hatua hiyo ni sehemu ya majukumu ya msingi ya Wizara yao katika kulinda haki na kuhakikisha upatikanaji wa haki sawa kwa wote.

Maleko amesema,katika maadhimisho hayo,Wataalamu wa sheria kutoka wizara hiyo ,wameunda timu maalum inayohudumia wananchi kwenye banda lao kwa kutoa elimu kuhusu masuala ya sheria,na kutoa msaada wa kisheria pale unapohitajika.

Aidha Maleko amesema, wizara hiyo imeanzisha dirisha maalum la huduma kwa wateja ambalo linasaidia kurahisisha upatikanaji wa huduma.

Kwa mujibu wa Maleko,kupitia dirisha hilo, wananchi hupewa namba maalum za mawasiliano ili waweze kufuatilia huduma hata baada ya maonyesho hayo kuisha kwa kupiga simu hiyo ili waweze kupata msaada pale wanapohitaji.