Judith Ferdinand,Timesmajira Online,Mwanza
Jeshi la Polisi Mkoa wa Mwanza katika kipindi cha Desemba 1 hadi 30,2024,limewafungia madereva 16,leseni za udereva kwa muda wa miezi sita.
Ikiwa ni ongezeko la madereva 10,ikilinganishwa na kipindi cha Desemba 1 hadi 31,2023,ambapo madereva 6,walifungiwa leseni za udereva.
Akizungumza Desemba 30,2024,mkoani hapa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza DCP.Wilbrod Mutafungwa,amesema,baada ya miezi hiyo sita kuisha madereva hao watapaswa kusomea tena udereva katika vyuo vinavyotambulika na kisha kurudi polisi ili wajaribiwe kama wameiva ili waweze kupata leseni upya.
Pia Mutafungwa,amesema katika kipindi cha Desemba 1 hadi 30,2024,jumla ya magari 17,ya kubeba abiria yalizuiliwa yasiendelee na safari,baada ya kukaguliwa na kubainika kuwa na ubovu.Mpaka wamiliki walipoyarekebisha na kukaguliwa ndipo yaliruhusiwa kuendelea na safari,lengo likiwa ni kulinda usalama wa wananchi.
Sanjari na hayo,amesema katika kipindi cha Desemba 1 hadi 30,2024,wamefanikiwa kupunguza uhalifu kwa asilimia 13,kupitia doria na misako inayoendelea,walifanikiwa kukamata makosa 2,525 na watuhumiwa 3,510 wa makosa ya jinai huku makosa hatarishi ya usalama barabarani 15,307 na watuhumiwa 14,851.
Ambapo ikilinganishwa na kipindi kama hicho cha Desemba 1 hadi 31,2023,makosa ya jinai yalikuwa 1,820 na watuhumiwa wa makosa ya jinai 2,215,huku watuhumiwa 13,320,wa makosa hatarishi ya usalama barabarani walikamatwa.
“Sawa na ongezeko ya la watuhumiwa wa makosa ya jinai 1,295 na watuhumiwa 1,522,wa makosa hatarishi ya usalama barabarani.Watuhumiwa wa makosa ya jinai kwa mwaka huu wamekamatwa kwa kujihusisha na vitendo vya uhalifu,kupatikana na mali zinazodhaniwa kuwa za wizi,kucheza Kamari,wizi,mauaji,ubakaji,ulawiti pamoja na kujihusisha na vitendo vya ukahaba,”amesema Mutafungwa.
Aidha,amesema,ongezeko hilo la makosa na watuhumiwa kukamatwa,linatokana na jitihada zinazofanywa na jeshi hilo mkoani kutokana na kuimarisha mifumo ya kiusalama pamoja na ushirikiano wa wananchi wanaoutoa kwa polisi.
More Stories
Madiwani Lushoto wameridhia bajeti ya bil 54.6 mwaka 2025/26
Kikao Mawaziri EAC,SADC kuleta matokeo chanya Congo
Kilosa waanza kuonja asali ya hewa ukaa