September 23, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Samaki sasa kufugwa kwenye majaruba ya mpunga

Na Mwandishi wetu, TimesMajira Online

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega amesema Wizara yake imeweka mkakati wa kuanza kufuga samaki katika mabwawa na majaruba ya mpunga ili kuongeza wigo wa upatikanaji wa samaki na kipato kwa wanachi.

Waziri Ulega amesema hayo wakati alipokitembelea Kikundi cha Ufugaji Samaki kwenye Mabwawa cha Mpitimbi B kilichopo, Mpitimbi, mkoani Ruvuma Septemba 21, 2024.

“Mwaka huu tuna mkakati wa kufuga samaki katika mabwana na majaruba ya mpunga lengo ni kueneza ujuzi kwa watu wengi zaidi waweze kufanya ufugaji huo ili kutanua wigo wa upatikanaji samaki na kujiongezea kipato pia”, amesema

Amesema kuwa Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe. Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan imedhamiria kuinua wananchi wake kupitia sekta za uzalishaji ikiwemo kuwezesha vijana wengi kuingia katika tasnia ya ufugaji samki ili wajikwamue kiuchumi.

Naye, Mkuu wa Wilaya ya Songea, Mhe. Wilman Kapenjama amesema mkakati huo ukifanikiwa utasaidia vijana wengi kuinuka kiuchumi na wao kama wilaya wako tayari kushirikiana na wizara kuhakikisha ufugaji wa samaki katika majaruba wanautekeleza ili wananchi wa sengea na viunga vyake wanakuwa na uhakika wa kupata kitoweo cha samaki wakati wote.