September 22, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Wanyakyusa wana jambo lao Septemba 27

Na Agnes Alcardo,TimesmajiraOnline,Dar

TAMASHA la Utamaduni wa Mtanzania Jamii ya Wanyakyusa, linatarajiwa kuanza Septemba 27 hadi 29, 2024 katika eneo la Kijiji Cha Makumbusho Kijitonyama Jijini Dar es salaam, lengo likiwa ni kuwakutanisha watu mbalimbali hususani wa jamii ya kinyakyusa pamoja na kuona na kujifunza mila na tamaduni za mnyakyusa.

Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Mbeya, Patrick Mwalunenge, anatarajiwa kuwa mgeni rasmi siku ya ufunguzi wa tamasha hilo, ambalo litafanyika kwa muda huo wa siku tatu, likitarajiwa kuhudhuliwa na watu zaidi ya 5000, kutoka ndani na nje ya Dar es Salaam.

Ambapo watu hao watapata fursa ya kujionea vitu mbalimbali vya asili ya jamii ya wanyakyusa ikiwa pamoja na Ngoma maarufu kama ‘ Mang’oma, muziki, vyakula vya asili, vinywaji ikiwemo pombe aina ya Kimpumu, Komoni, Kyindi na nyumba zinazoakisi uhalisia wa jamii ya watu wa Mkoa wa Mbeya.

Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi, Enelyn Mwakapila, amewaomba wananchi wote hususani wa jamii ya kinyakyusa kujitokeza kwa wingi kuhudhuria katika tamasha hilo, akisema kuwa kufanya hivyo kunakuza hadhi na kuheshimisha tamaduni za makabila ya Tanzania.