September 21, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

CCM yapongeza hotuba ya Rais Samia

Na Agnes Alcardo, Timesmajira Online. Dar

CHAMA Cha Mapinduzi (CCM), kimempongeza Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa hotuba yake aliyoitoa hivi karibuni Mkoani Kilimanjaro ya kukemea vitendo vya utekaji na mauaji, huku akiliagiza Jeshi la Polisi kufanya uchunguzi wa kina kubaini wanao husika na vitendo hivyo huku kikilaani vitendo vya upotoshaji vinavyofanywa na baadhi ya vyama pinzani vya uchochezi na uvunjifu wa amani kupitia hotuba zao hususani chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA).

Pia, amesema, CCM imejipanga vizuri kushinda kwa kishindo Uchaguzi wa Serikali za Mitaa kutokana na maandalizi makubwa yaliyofanywa na kazi nzuri iliyofanywa na Rais Dk.Samia ya kutekeleza miradi mikubwa na kupeleka fedha nyingi vijijini za utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

Pongezi hizo zimetolewa leo Septemba 22, 2024 na Katibu wa NEC, Itikadi, Uenezi na Mafunzo wa CCM Taifa, CPA Amos Makalla, alipokuwa akizungumza na Wajumbe wa Kamati ya siasa Mkoa wa Dar es Salaam.

“Mheshimiwa Rais alitoa kauli ile, akiwa Rais, kiongozi mkuu wa nchi na Amiri jeshi Mkuu, lakini watu wenye nia mbaya wamekuwa mitandao na wengine katika vikao vyao wakipotosha na kuipa maana nyingine kauli Ile.

“Nataka niseme Mheshimiwa Rais Baada ya taarifa za kifo Cha Kibao, alitoa pole na kutoa maagizo ya kufanyika uchunguzi wa kina, alitoa pole Kwa masikitiko makubwa tofauti na wengine wanavyo potosha kauli na maagizo ya Rais Dk.Samia,” amesema.

Ameongeza “CCm kupitia Mwenezi nilitoa pole na siku hiyo Rais alitoa pole na maelekezo ya uchunguzi wa kina kwa kusikitishwa na kifo hicho, vivyo kwa Rais na Watanzania wote Kila mmoja hili jambo lilimshtua na alitaka lisijirudie tena, inapotoke jambo la kifo wote linatusikitishaa,” amesema.

Ameongeza kuwa, jambo ambalo limeleta mtazamo tofauti kwa wanaoitakia mema nchi yao na CCM ni baada ya kuona hotuba Ile kugeuza maana na kuwepo kwa upotoshaji na kauli zingine ambazo hazina maana, huku akitolea mfano wa Chama kimoja Cha upinzani kupitia Mwenyekiti wao wamekuwa wakitoka kauli tofauti za kutokubaliana na uchunguzi.

Aidha amesema kuwa, CCM katika kuhakikisha inashinda kwa kishindo katika uchaguzi wa Serikali za Mitaa, itahakikisha inawaletea wananchi wagombea safi na wasio na makandokando, huku akiwataka wananchi kwa ujumla kuendelea kukiamini chama cha CCM huku akisema kuwa, lengo la vyama pinzani kukichafua chama cha CCM ni moja ya njia ya kuficha migogoro yao iliyopo ndani ya chama.

“Tunajua ipo mikakati inayofanywa na baadhi ya vyama pinzani ambayo walianza na maandamano wakagundua kuwa wananchi wengi hawaungi mkono hivyo wameanza kukatakata hotuba ya Rais na kuiletea maana nyingine ili tu walete sintofahamu kwa wananchi, lakini wananchi siyo wajinga”, ameongeza Makalla.