September 20, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Rais Samia kufungua Mkutano wa  Wenza wa Marais, Wawaziri

Na Jackline Martin

RAIS  Samia Suluhu Hassan anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika Mkutano wa 11 wa Taasisi ya Merck Foundation Asia Afrika Luminary ambao utafungua njia ya utekelezaji wa ahadi mpya zitakazotolewa na wenza wa marais,  mawaziri na Timu ya Merck Foundation .

Lengo ni   kuhakikisha upatikanaji wa suluhisho bora na usawa wa huduma za afya za watu wa Afrika hususan kutoka nchi ambazo zitakuwepo katika mkutano huo ikiwa ni pamoja na Tanzania.

Mkutano huo pia utatumika kama jukwaa la kuchukua hatua mahususi katika kushughulikia unyanyapaa na mtazamo wa kijamii wa utasa,  kuboresha upatikanaji wa huduma ya uzazi salama  na zenye ufanisi kwa wanawake na wasichana Barani Afrika.

Akizungumza na waandishi wa habari jana Jijini Dar es Salaam, Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Dorothy Gwajima alisema mkutano huo utafanyika kwa mara ya 11 na mara ya kwanza nchini Tanzania.

Kwa mujibu wa waziri huyo mkutano huo utafanyika Oktoba 29 na 30, 2024, ambapo mikutano 10 iliyotangulia ilifanyika katika nchi za  za Ujerumani,  Kenya , Ivory Cost ,  Misri,  Mauritius, Senegal,  Ghana, Zambia , Umoja wa Falme za Kiarabu na   India.

“Tuinachukua fursa hii adhimu kumshukuru sana Rais Dkt. Samia kwa kukubali ombi hilo, hivyo kuwezesha Tanzania kupata heshima hiyo kubwa ya kuwa mwenyeji wa Mutano huo wa kimataifa kwa mara nyingine.”

Alisema pamoja na mambo mengine, Mkutano huo utajadili mada nne za kitaalam pamoja na mada moja kuhusu mafunzo kwa vyombo vya Habari

“Mada zitakazojadiliwa ni kuhusu afya ya Mama na Mtoto,  Ugonjwa wa Saratani, Ugonjwa wa Kisukari na Shinikizo la damu, Mipango ya Maendeleo na kujengewa uwezo na mafunzo kwa vyombo vya habari vya afya.”

“Washiriki wa Mkutano huu watanufaika na maarifa na uzoefu unaotolewa na wataalamu mbalimbali na watafiti ambao watazungumza kwa kina kuhusu mada tajwa hapo juu kwa lengo la kuongeza uelewa wa jamii juu ya masuala mbalimbali ya afya ikiwa ni pamoja na Magoniwa yasiyo ambukiza, matatizo ya kupumua, na mengineyo.”

Waziri Gwajima alizitaja sababu mbalimbali zilizopelekea mkutano huo kufanyika nchini ikiwemo jitihada za wazi za Serikali ya Awamu ya Sita na awamu zilizotangulia za kuwekeza katika sekta ya afya, hasa afya ya akina mama na watoto, ambavyo vimeifanya Tanzania kufanya vizuri katika utekelezaji wa malengo ya maendeleo ya kimataifa yakiwemo ya Milenia na Maendeleo Endelevu.

Pia alisema  Tanzania  imechaguliwa kutokana na mazingira mazuri ya amani na utulivu, ambapo washiriki wa mkutano huo, hususan viongozi mbalimbali watapata nafasi ya kutekeleza jukumu la kushiriki kwenye mkutano kwa amani na utulivu. 

“Sifa nyingine ni ongozi bora na wa kupigiwa mfano wa Serikali inayoongozwa na  Dkt. Samia, ambaye amendela kupaisha diplomasia ya Tanzania, ikiwemo diplomasia ya mikutano kama hiyo ya kimataifa.”

Aidha alisema Mkutano huo unategemewa kuwa na washiriki takribani 600  wakiwemo “Wenza wa Marais kutoka nchi za Afrika ambazo ni Angola,  Botswana,  Burundi, Ivory Cost, Cape Verde, Afrika ya Kati, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC),  Gambia,  Ghana, Kenya,  Liberia,  Malawi  na Mauritania. 

“Nyingine ni Msumbiji, Nigeria, São Tomé na Príncipe,  Sierra Leone,  Rwanda,  Afrika Kusini,  Comoros,  Eswatini,  Zambia,  Zimbabwe na mwenyeji, Tanzania, ambapo tutawakilishwa na Mwenza Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mama Mariam Mwinyi.”

“Mawaziri wa Afya, Jinsia, Mawasiliano, Elimu, Ustawi wa Jamii kutoka nchi zilizoalikwa nao pia watahudhuria, wajumbe wa 45 wataalam watakaoambatana na wenza wa Marais kutoka nchi tajwa, wataalamu wa huduma za afya 500, wasomi, watunga sera na waandishi wa habari, Mabalozi wanaowakilisha nchi ambazo wenza wa Marais wamealikwa na Mabalozi wa Tanzania kutoka nchi hizo pia watahudhuria Mkutano huo

Waziri Gwajima alisema kufanyika kwa Mkutano huo chini Tanzania kutaleta faida na manufaa makubwa kwa nchini ya Tanzania  ikiwa ni pamoja na kuongeza uelewa kwa Watanzania kuhusu masuala ya afya kufuatia mkutano kufanyika chini.

Mkurugenzi Mtendaji wa Merck Foundation, Dkt. Rasha Kelej alisema tayari washiriki wakiwamo wake wa Marais ambao ni mabalozi wa Merck Foundation wameridhia kuhudhuria mkutano huo lakini pia watafiti nguli wa masuala ya afya ya uzazi, saratani, kisukari na shinikizo la damu watahudhuria na kuwasilisha mada mbalimbali zitakazojadiliwa.

Aidha alisema wataendelea kushirikiana na nchi mbali mbali ikiwemo kusomesha wataalaam wa afya kupitia program ya kutoa scholarship.