September 20, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Dkt.Mpango ahimiza kasi ya upandaji miti kuongezwa

Na Joyce kasiki,Timesmajira online,Dodoma 

MAKAMU wa Rais Dkt.Philip Mpango amesema kuwa kasi ya upandaji miti bado ni ndogo kuliko kasi ya ukataji miti huku akieleza kuwa hayo yote yanasababishwa na wananchi kutokuwa na elimu  ya kutosha juu ya athari za mazingira.

Dkt. Mpango amesema hayo jijijni Dodoma  wakati akifungua mkutano maalum wa viongozi,wataalam na wadau kuhusu mwenendo wa hali ya mazingira nchini huku akisema  namna ya kutoa elimu kwa umma haiendi ipasavyo kwa  wananchi .

Amewataka  wataalam  husika kujitazama upya na kuona  mbinu sahihi ya kuitumia  ili elimu iweze kuwafikia wananchi na kuongeza uelewa zaidi kuhusu utunzaji wa mazingira. 

Amesema kuwa suala la usimamizi na utunzaji wa mazingira ni kipaumbele katika maendeleo ya nchi, hata hivyo taarifa ya 4 ya mazingira inaonesha kuwa hali ya utunzaji wa mazingira nchini hairidhishi. 

“Taifa letu,nchi yetu hivi sasa inalia,ninasema inalia kwa sababu athari za uhatibifu wa mazingira na mabadiliko ya tabia nchi ni nyingi,nikubwa sana,zimetuathiri kwa kiasi kikubwa sana,zinahatarisha uhai wa viumbe vyote ikiwe sisi wanadamu, 

“Inahatarisha upatikanaji wa maj,inahatarisha usalama wa chakula lakini pia inatuongezea magonjwa tena mengine ya mlipuko ndiomana tunalia nchi yetu inalia,”amesema Dkt.Mpango

Kwa upande wake Waziri wa Nchi,Ofisi ya Makamu wa Rais(Muungano na Mazingira)Dkt.Ashatu Kijaji amesema kuwa Lengo la Mkutano huo ni kuendelea kuongeza uelewa wa Viongozi na Wataalamu kutoka Sekta ya Umma, Sekta Binafsi na Mashirika yasiyo ya Kiserikali kuhusu mwenendo wa hali ya mazingira na hatua zinazopaswa kuchukuliwa ili kuimarisha uhifadhi na usimamizi wa mazingira. 

Vile vile, Mkutano huo unalenga kuongeza hamasa na ushiriki wa wadau wote katika kukabiliana na changamoto za uharibifu wa mazingira na mabadiliko ya tabianchi. 

“Katika Mkutano huu, mada mbalimbali zitawasilishwa,Mada hizo zinahusu masuala mbalimbali yakiwemo Mwenendo wa Hali ya Mazingira nchini, Biashara ya Kaboni na mchango wake katika kukabiliana na mabadiliko ya Tabianchi,Wajibu wa Wizara, Taasisi za Umma, Sekretarieti za Mikoa, Mamlaka za Serikali za Mitaa, Sekta Binafsi na Asasi za Kiraia katika usimamizi wa Mazingira,Uchumi wa Buluu na Tafsiri yake katika Ujenzi wa Taifa,Ugharamiaji wa Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira, na Mabadiliko ya Tabianchi.”

Aidha amesema, katika Mkutano huu kutakuwa na mafunzo kuhusu mbinu za kuhimili mabadiliko ya tabianchi ambayo yataendeshwa na Shirika la Umoja wa Mataifa la Maendeleo (UNDP) ambapo  washiriki watapata fursa ya kutoa maoni yao katika masuala mbalimbali yatakayowasilishwa na aliwataka  Washiriki watoe maoni yao kwa uwazi na uhuru.

Naye Waziri wa Nchi,Ofisi ya Makamu wa kwanza wa Rais Zanzibar Harusi Said Suleiman amesema kuwa zanzibar kwakuwa ni sehemu ya dunia imeathirika na tabia nchi na pia imethirika kidogo kimazingira. 

Amesema kuwa serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imekuwa ikitoa mashirika katika sekta mbalimbali ikiwemo sekta ya mazingira. 

“Hivi karibuni mwezi wa 8 tulizindua program kubwa ya kuirisisha zanzibar ya kijani,program hii inadhamira ya kuirudisha zanzibar katika hali ya uhalisia uliokuwa yaani rangi ya kijani,  na tangu tuizindue vimeshajitokeza vikundi mbalimbali na vingine vimeshaanza kutekeleza upandaji na usimamizi wa miti mbalimbali mana lengo sio kupanda tu bali ni kusimamia na kuhakikisha vinakuwa katika hali ambayo tunaitegemea,”amesema Said