October 7, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

CPA Makalla awataka wananchi wa Kigamboni kuipatia ushindi wa kishindo CCM, uchaguzi Serikali za Mitaa


Na Agnes Alcardo, Timesmajira Online. Dar

KATIBU wa NEC, Itikadi, Uenezi na Mafunzo (CCM) Taifa, CPA Amos Makalla, amewataka wananchi Kigamboni kuendelea kukiamini na kukipatia ushindi wa kishindo kwa kura nyingi Chama cha Mapinduzi (CCM) katika uchaguzi wa Serikali za Mitaa utakaofanyika Novemba 27, 2024.

Amesema, zipo sababu kuu tatu za kuweza kukipatia ushindi chama hicho ikiwa ni pamoja na utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM 2020/2025, uongezaji wa Wanachama wapya kutoka vyama pinzani na vyama pinzani kupoteza muelekeo.

CPA Makalla, amesema hayo leo, Agosti 27, 2024 Jijini Dar es Salaam kwenye Mkutano wa hadhara uliofanyika katika Viwanja vya Tungi Mnadani, Wilayani Kigamboni.

“Kuna kila sababu ya CCM kuendelea kushinda kwani inatekeleza Ilani yake kwa kuendelea kuwahudumia wananchi wake, kwani kila sehemu kuna miradi ya maendeleo, hvyo utekelezaji tu wa Ilani unatosha kutupatia ushindi.

“Lakini pia, sababu nyingine ya kutupatia ushindi CCM ni kutokana na imani kubwa ya wananchi kwetu ambao wamekuwa wakihamia CCM wakitokea vyama pinzani kutokana na vyama hivyo kupoteza muelekeo”, amesema Makalla.

Aidha amesema kuwa, mafanikio yanayopatikana ndani ya CCM yanatokana na ushirikiano wa viongozi wote wa ngazi za juu na chini.

Pia, amesema, amani na utulivu uliopo CCM unatokana na muunganiko wa wenyeviti wa vitongoji, wenyeviti wa serikali za Mitaa na Serikali kwa ujumla.