October 6, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Tundu Lissu atua jijini Dar, apata mapokezi ya kishindo

Na Mwandishi Wetu, TimesMajira Online, Dsm

MAKAMU Mwenyekiti wa CHADEMA (Bara) Tundu Lissu, amewasili nchini akitokea Ubelgiji alipokuwa kwa matibabu baada ya kushambuliwa kwa risasi na watu wasiojulikana Septemba 7, mwaka 2017.

Lissu amewasili kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere jijini Dar es Salaam mchana huu na kupokelewa na viongozi wa juu wa chama wakiongozwa na Mwenyekiti wa CHADEMA Taifa, Freeman Mbowe na Katibu Mkuu, John Mnyika.

Lissu ametoka ndani ya Uwanja huo wa ndege saa 8:20 baada ya kumaliza taratibu zote na alipotoka nje alipokelewa kwa shangwe na maelfu ya wafuasi wa CHADEMA.

Akionekana mwenye bashasha Lissu alianza kuwapungia mkono wananchi hao, huku mkono wake ukiwa umeshika gongo moja tofauti na Mbowe ambaye alikuwa akitembea kwa msaada wa magongo yake mawili.

Mbowe aliumia hivi karibuni jijini Dodoma na kulazwa mkoani humu, kabla ya kuhamishiwa Hospitali ya Agha Khan, jijini Dar es Salaam kwa matibabu zaidi.

Baada ya kuonekana hadharani shangwe na vigelegele vilianza kutoka miongoni mwa maelfu ya wana CHADEMA na yeye aliitikia shangwe hizo kwa kutoa sakafu yake na kuanza kuwapungia, kitendo kilichoamusha shangwe zaidi.

Alianza safari yake ya kutoka Uwanja wa Ndege akiwa kwenye gari la wazi, huku akiendelea kuwapungia watu mkono kama ishara.

Mbali na Mbowe na Mnyika, viongozi wengine waliojitokeza kumpokea ni pamoja na wabunge mbalimbali waliomaliza muda wao. Baadhi ya wabunge hao ni Godbless Lema, Mchungaji Peter Msigwa, Joseph Haule, Joseph Mbilinyi (Sugu), John Heche, aliyekuwa Meya wa Ubungo, John Jacob

www.timesmajira ilishuhudia utulivu mkubwa wakati wa kupokewa kwa Lissu, huku wananchi waliojitokeza wakiwa na mabango yaliyokuwa na ujumbe mbalimbali.