September 22, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Rais Dkt.Samia kufanya ziara siku tatu Katavi

Na George Mwigulu,Timesmajiraonline, Katavi.

RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Taifa,Dkt.Samia Suluhu Hassan anatarajia kufunga kilele cha wiki ya Jumuiya ya Wazazi wa chama hicho pamoja na kufanya ziara ya kikazi katika Mkoa wa Katavi.

Mkuu wa Mkoa wa Katavi, Mwanamvua Mrindoko akitoa taarifa hiyo Julai 10, 2024 ofisini kwake mbele ya Wanahabari amesema kuwa Rais atafika mkoani humo Julai 12, 2024 na kufanya ziara ya kikazi hadi Julai 15, 2024.

Mrindoko amesema kuwa Julai 12, 2024 Rais Dk Samia licha ya kuwasili katika uwanja wa ndege Mpanda atatembelea jengo la abiria uwanjani hapo.

Ameeleza kuwa akiwa Mkoani Katavi atakuwa mgeni rasmi kwenye kilele cha wiki ya Jumuiya ya Wazazi kitaifa ambayo itafungwa Julai 13, 2024 rasmi katika uwanja wa CCM Azimio manispaa ya Mpanda.

“Kwenye kilele cha maanzimisho ya wiki ya wazazi Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan atazungumza na wananchi wa mkoa wa Katavi kupitia mkutano wa hadhara” Amesema Mrindoko.

Vilevile atakagua kituo cha kupozea umeme wilaya ya Mlele ambapo umeme wa gridi ya taifa kutoka Mkoa wa Tabora utapokelewa na kupozwa kwa ajili ya matumizi mbalimbali.

Julai 14, 2024 ameeleza kuwa Rais atafungua jengo jipya la ofisi ya Kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Katavi na kufanya uzinduzi wa maghala ya kutunzia mazao katika eneo la Mpanda Hotel yanayo milikiwa na taasisi ya serikali ya NFRA.

Aidha Julai 15, 2024 anatarajiwa kutembelea ujenzi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Katavi ambapo atahitimisha kusalimiana na wananchi wa kijiji cha Kibaoni halmashauri ya wilaya ya Mpimbwe.

Mkuu wa Mkoa huyo amewaomba wananchi wa Mkoa wa Katavi kundelea kuimarisha amani na utulivu huku akiwaomba kujitokeza kwa wingi.