October 6, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Kissaga:Tanzania ,Iran unganisheni nguvu za pamoja kufanya biashara

Na Mwandishi wetu, Timesmajira

MKURUGENZI Mtendaji wa Chemba ya Biashara,Viwanda na Kilimo (TCCIA),Oscar Kissaga amesema kuna umuhimu wa Watanzania  kuunganisha nguvu za pamoja na wafanyabiashara wa Jamhuri ya Kiislam ya  Iran  kufanyabiashara kwa pamoja na kuunda mtandao utakaoweza kufikia soko la Dunia.

Akizungumza leo jijini Dar es Salaam wakati alipohudhuria siku maalum ya Iran ndani ya maonesho ya 48 ya biashara ya kimataifa ”Sabasaba”yanayofanyika katika viwanja vya Mwalimu Nyerere,amesema siku hiyo ni muhimu kwa watanzania katika kujifunza na kuona ni fursa gani ambazo watu wa iran wanazo na kuweza kuzifanyia kazi.

Amesema kupitia mkutano huo,wafanyabiashara wa Iran wameweza kuonesha fursa mbalimbali ambazo zinapatikana nchini kwao ikiwemo Kilimo,Utafiti na Maendeleo hususan katika dawa za Mifugo na Binadamu.

”Natoa wito kwa watanzania na wanachama wa TCCIA, kujiunganisha na kuangalia fursa zilizopo kwa wafanyabiashara wa Iran katika maonesho haya na kuzifanyia kazi,”amesema na kuongeza

”Huwezi kufanya jambo pekee yako,naamini ukiunganisha nguvu za pamoja na wenzetu wa Iran na uhakika tunaweza kufanya biashara za uhakika na kuunganisha mtandao ambao utatufikisha katika soko la dunia,”amesema.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TANTRADE),Latifa Khamis amesema Jamhuri hiyo ya Kiislam ya Iran imeonesha utayari wa kukuza ushirikiano na Tanzania katika kuhamasisha teknolojia zao  mbalimbali.

Akitaja miongoni mwa teknolojia hizo ni pamoja na sekta ya afya,Kilimo na Tafiti za Uendelezaji ,Dawa za Mifugo na Binadamu pamoja na utengenezaji wa Chanjo mbalimbali.

”Hatua hii itachochea zaidi ukuaji wa matumizi ya teknolojia nchini katika shughuli mbalimbali za uzalishaji,”amesema.

Aidha amesema Iran ni wataalam wa utengenezaji wa aina mbalimbali za chanjo hivyo wamehaidi kuhamisha teknolojia yao na kuwafundisha watanzania kuweza kuzalisha  ”Kupitia mkutano huu utaweza kuzaa matunda mazuri ambayo na sisi tutaweza kutengeneza chanjo zetu mbalimbali,natoa wito kwa watanzania kushiriki katika programu hizi kwani zinatija katika biashara zetu ikiwa tunatembea na kuondoka na fursa katika maonesho haya,”amesema.

Kwa upande wake Balozi wa Iran nchini Tanzania,Hussein Bahineh amesema uhusiano katika sekta mbalimbali umeendelea kukua tangu mwaka 1979 mataifa haya yalipoanza kushirikiana na kidiplomasia.