October 9, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Wataka katiba mpya iwe msaada kwa wenye ulemavu

Na Esther Macha, Timesmajira Online, Mbeya

WADAU na wananchi jijini Mbeya wameombwa kuendelea kutilia mkazo uwepo wa suala la Katiba Mpya kuzungumzia watu wote hususani kundi la watu wenye ulemavu na sio kuzungumzia viongozi pekee waliopo madarakani.

Kauli hiyo imetolewa Juni 8,2024 na Doreen Mayami kutoka shirika lisilo la kiserikali linalojishughulisha na watoto wenye ulemavu (CST)wakati wa mjadala wa wazi ulioandaliwa na Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS)kwa ajili ya kupata kattiba Mpya Tanzania uliofanyika jijini Mbeya.

Doreen Mayami kutoka Child Support Tanzania

Mayami amesema kuwa katiba iliyopo haizungumzi kwa uwazi masuala ya watu wenye ulemavu ambapo ipo tofauti na nchi zingine.

“Ukilinganisha na katiba ya wenzetu mfano Kenya ,South Africa katiba zao zinawazungumzia watu wenye ulemavu na unaposema ubaguzi kwa katiba za wenzetu zimetaja kundi hilo moja kwa moja lakini kwa katiba ya Tanzania haijamtaja mtu mwenye ulemavu moja kwa moja,”amesema Mayami.

Hata hivyo Mayami amesema watu wenye ulemavu wamekuwa wakiptia changamoto mbalimbali na kusababisha kushindwa kuyafikia yale wanayotamani.

Kwa mujibu wa Mayami amesema kuwa u kwenye Rasimu ya Warioba mapungufu yote yaliyopo katika katiba ya sasa yamezungumzwa na kuwekwa wazi hivyo ni jukumu la kila mtanzania kuendelea kuipigia kelele ili kuweza kupata katiba mpya ambayo itazungumzia watu wote hususani kundi la watu wenye ulemavu na si viongozi pekee waliopo madarakani.

“Katiba ya sasa ibara ya 11 inazungumzia masuala ya kazi,elimu na inaonesha kipengele cha kazi na elimu lakini watu wenye ulemavu hawana uwezo wa kupinga kwenye vyombo vya sheria na kama katiba haijatoa nafasi kwa hili kundi wanapataje haki katika nchi yao alihoji Mayami ?

Jimmy Ambilikile kutoka Chama cha watu wenye ulemavu Mkoa wa Mbeya (CHAWATA)amesema kuwa sura ya pili ya Katiba inasema atakayeruhusiwa kugombea na nafasi ya uongozi ni mtu yeyote kikubwa awe ameruhusiwa na chama chake lakini kumekuwa na dhana tofauti kwa watu wenye ulemavu kwa kutoangaliwa kwenye vyama vya siasa ambapo wamebaki kuangalia ulemavu wao na uwezo walionao hivyo katiba mpya ni muhimu ili yote yafanyike.

Hata hivyo Wakili wa kujitegemea kutoka TLS Aminaeli Zephania amesema kuwa suala la katiba mpya halipingiki kwasababu watanzania wote wanahitaji kwani ni chombo ambacho kinaishi lazima kitatue matatizo yaliyopo wakati uliopo na ujao.

Mmoja wa wanasiasa walioshiriki Joseph Mbilinyi (Sugu)

Aidha Zephania amesema kuwa katiba inayotumika ni ya muda mrefu kiasi kwamba haikidhi mahitaji ya wakati huu uliopo na mwingine na kwamba hata Rasimu inayozungumziwa haijakidhi mahitaji yote hivyo hitahi la Katiba mpya ni muhimu.

Baadhi ya wadau walioshiriki mjadala huo