April 30, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Walimu wakicheza kuonyesha mtoto wa darasa la awali hujifunza zaidi kwa kucheza

Mtaalam aanika mbinu za kuwajengea msingi mzuri watoto

Na Joyce Kasiki, TimesMajira Online, Chamwino

WAZAZI na walezi wameshauriwa kuwajengea watoto misingi mizuri tangu wakiwa na umri wa kuanzia miaka 0-8 kwa kuwa kipindi hicho, ndicho mtoto anaelewa mambo kwa haraka.

Hayo yamesemwa na Mkufunzi wa Shirika la Kusaidia Watoto wanaopitia Changamoto mbalimbali (CiC) Frank Samson, wakati akitoa mada kwa walimu wa madarasa ya awali wilayani Chamwino mkoani Dodoma kuhusu makuzi ya awali kwa binadamu.

Amesema katika kipindi hicho ndio wazazi na walezi wanaweza kufundisha watoto mambo mema au mabaya kutegemeana na mazingira wanayoishi na baada ya hapo fursa ya kumjenga mtoto katika mambo mbalimbali inazidi kupungua.

Mkufunzi huyo amesema katika kipindi hicho mtoto anajengwa vizuri katika lugha, hisia, kiakili, kimwili, kiutamaduni na kujongea.

Walimu wa madarasa ya awali wa wilayani chamwino wakiwa katika makundi wakichambua Sera kuhusu ujifunzaji wa Elimu ya awali

“Katika umri wa miaka 0-8 ndio misingi ya mwanadamu unajengwa,akivuka umri huo fursa ya kumjenga katika mambo mbalimbali inazidi kupungua,” amesema Frank na kuongeza;

“Lakini katika umri huo ndio mtoto anaweza kujifunza mambo mabaya, unakuta wazazi wanagombana, wanatukanana matusi kila siku, ni lazima mtoto huyu atajifunza kutukana.”

Lakini pia Frank amesema,mtoto katika umri huo hujifunza kupitia milango mitano ya fahamu ambayo ni pua(kunusa),sikio (kusikia),mkono (kugusa),jicho (kuona) na ulimi (kuonja).