October 6, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

NEC yaanza kuweka wazi daftari la wapiga kura

Na Hadija Bagasha, TimesMajira Online, Tanga

TUME ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) imeanza rasmi kuweka wazi daftari la kudumu la awali la wapiga kura ambapo watafanya uhakiki na urekebishaji wa taarifa za wapiga kura kwa nchi nzima.

Mchakato wa ubandikaji wa daftari la kudumu la wapiga kura utadumu kwa muda wa siku nne kuanzia tarehe 17 mipaka 20 ambapo wananchi watapata wasaa wa kwenda kurekebisha taarifa zao.

Awali akizungumza na waandishi wa habari mkoani Tanga ofisa habari mwandamizi kutoka NEC, Zawadi Masala, alisema wamekuja kuweka wazi daftari hilo la awali la kudumu la wapiga kura ili kuhakikisha wanapata daftari ambalo ni safi.

Alisema njia zitakazotumika kuweka wazi daftari hilo ni kulibandika katika kila kituo kilichotumika wakati wa uboreshaji wa daftari la kudumu la wapiga kura ambapo wananchi watapata nafasi ya kuweza kwenda kuangalia taarifa zao kwa kufanya uhakiki wa taarifa zao.

Zawadi alisema baada ya kufanya uhakiki mwananchi atakapokuta taarifa zake zina makosa urekebishaji wa taarifa hizo utafanyika katika ngazi ya Halmashauri katika vituo maalumu.

Alisema kwa sasa tume haiboreshi taarifa za wapiga kura, lakini inarekebisha taarifa za wapiga kura na endapo mwananchi atakuta taarifa zake zina kasoro yeyote ni muda muafaka wa kuweza kuzirekebisha katika Halmashauri husika.