October 6, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Watumishi 16 wa Ikulu Kenya, Magavana wabainika kuwa na Corona

Na Mwandishi Wetu, TimesMajira Online, Nairobi

Idadi ya watumishi wa Ofisi ya Rais katika Ikulu ya Jamhuri ya Kenya iliyorekodiwa kwa kubainika kuwa na virusi vya Corona (Covid-19) imefikia 16 hadi sasa.

Hayo ni kwa mujibu wa taarifa iliyoripotiwa na vyombo vya habari nchini humo ikiwemo tovuti ya People.

Vyanzo vya habari ambavyo havikutaka majina yao kuchapishwa kutoka ndani ya Ikulu vimebainisha watumishi wanne wapo ndani ya Ikulu hadi sasa na wengine wameshapelekwa karantini.

“Kwa sasa tuna watumishi 16 ndani ya Ikulu ambao wamebainika kuwa na virusi vya Corona, wanne kati hao wapo ndani ya Ikulu na waliosalia wapo nje ya maeneo ya Ikulu,” kimebainisha chanzo kutoka Ikulu ya Kenya.

Haya yanajiri siku chache baada ya maafisa waandamizi ndani ya Ikulu kukimbizwa kwenda hospitali binafsi jijini Nairobi kufanyiwa uchunguzi na kugundulika wameambukizwa.

Pia usiku wa juzi.Imeripotiwa kuwa, magavana waliotembelea Ikulu ya Rais wengi wao baada ya vipimo wamebainika kuwa na Corona.

Awali, Msemaji wa Ikulu ya Kenya, Kanze Dena amenukuliwa akisema kuwa,wanafamilia wote wa watumishi waliobainika na virusi wanafuatiliwa kwa karibu.

Amesema, Serikali imechukua hatua kadhaa ikiwa ni pamoja na kuwapeleka watumishi wanaogundulika kuwa na Corona katika Hospitali ya Rufaa ya Chuo Kikuu ya Kenyatta iliyopo katika kauti ya Kiambu kwa matibabu zaidi.