October 5, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Uchaguzi DOREFA kufanyika Novemba 29

Na Nuru Mkupa, TimesMajira Online, Dodoma

UCHAGUZI mkuu wa Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dodoma (DOREFA) umepangwa kufanyika Novemba 29 mwaka huu chini ya kamati ya Uchaguzi ya Shirikisho la Soka nchini (TFF).

Akitoa taarifa ya uchaguzi huo, Kaimu Mwenyekiti wa Kamati ya Uchaguzi, Wakili Benjamin Kalume amesema kuwa, TFF itasimamia uchaguzi huo baada ya chama hicho kutokuwa na Kamati ya uchaguzi baada ya ile iliyokuwepo kumaliza muda wake.

Pia Kamati ya Utendaji ilishindwa kuteua Kamati ya Uchaguzi kwa mujibu wa sheria baada ya muda kupita jambo ambalo sasa litafanya Kamati ya Uchaguzi ya TFF kusimamia uchaguzi huo.

Nafasi ambazo zitagombaniwa katika uchaguzi huo ni nafasi ya Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti, Katibu, Katibu Mkuu na Katibu Msaidizi, Mweka hazina, Mjumbe wa Mkutano Mkuu, Mjumbe wa Mwakilishi wa klabu pamoja na wajumbe watatu wa Kamati ya Utendaji.

Fomu kuelekea katika uchaguzi huo zimeanza kutolewa leo na zoezi hilo litafungwa Novemba 15 ambapo gharama itakuwa Sh. 200,000 na kwa wajumbe na Kamati ya utendaji itakuwa Sh. 100,000 kupitia akaunti ya DOREFA.

“Tunawaomba wadau wa Mpira ndani ya Mkoa wa Dodoma kujitokeza kwa wingi kuchukua fomu za kugombea nafasi hizi zilizotangazwa kwa Katibu wa DORAFA kuelekea kwenye uchaguzi wetu tutakaoufanya Novemba 29,” amesema Wakili Kalume.