October 5, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Wafanyabiashara Dodoma wampongeza Rais Magufuli

Na Joyce Kasiki,TimesMajira online,Dodoma

BAADHI ya wafanyabiashara jijini Dodoma wamempongeza Rais Dkt.John Magufuli kwa kupata ushindi wa kishindo katika uchaguzi Mkuu uliofanyika Oktoba 28, mwaka huu.

Wakizungumza na mtandao huu kwa nyakati tofauti wafanyabiashara hao wamesema ushindi huo wa Dkt.Magufuli ni kutokana na kazi kubwa aliyoifanya ya kuwaletea wananchi maendeleo.

Godfrey Makoi mmoja wa wajasiriamali wanaofanya biashara mkoani Dodoma

Godfrey Makoi mkazi wa jiji la Dodoma amesema Watanzania wamemchagua Dkt.Magufuli kutokana na uchapakazi wake lakini pia kuleta maendeleo ya wananchi na Taifa kwa ujumla.

Makoi ambaye ni mmiliki wa GM Pub iliyopo maeneo ya Dodoma Inn jijini Dodoma amesema,ushindi huo ni kielelezo tosha kwamba wananchi wamekubali kazi kubwa aliyoifanya Rais huyo kwa kipindi kifupi cha miaka mitano aliyokaa madarakani.

“Viongozi wengi wamepita wamefanya kazi nzuri tunawashukuru lakini Rais wetu Dkt.Magufuli amefanya vizuri zaidi tena kipindi kifupi,bado naamini katika kipindi hiki cha miaka mitano mingine atafanya vizuri zaidi ikiwa ni pamoja na kumalizia na kutekeleza ahadi alizotuahidi wananchi akiwa katika kampeni za uchaguzi.” amesema.

Amewasihi vijana kubuni na kufanya kazi za kuwaingizia kipato ili kuunga mkono jitihada za Serikali za kuondokana na umasikini badala ya kukaa vijiweni kwa kisingizio cha kukosa ajira Serikalini.

Joseph Jumanne mkazi wa Kisasa ametumia fursa hiyo kumuomba Rais Dkt.Magufuli aendelee kuwajali wanyonge kama ambavyo amekuwa akijipambanua kwamba yeye ni Rais wa wanyonge.

Jumanne ambaye ni mfanyabiashara wa matunda amesema Rais Magufuli amekuwa akiwajali wanyonge wakiwemo wafanyabiashara ndogo ndogo ambao wameishi na kufanya kazi zao kwa kipindi cha uongozi wake bila kubughudhiwa tofauti na awamu nyingine za uongozi.

“Sisi wananchi wa hali ya chini tunapata kipato katika biashara hizi hizi ndogo ndogo na ndio zinatuwezesha kujikimu na familia zetu,tunasomesha watoto lakini pia tunajenga hadi nyumba,hii ni kutokana na kufanya biashara zetu kwa kutumia” amesema Jumanne.

Amemuomba Rais Magufuli aendelee kuwajali kwa kuhakikisha wanaendelea kufanya biashara zao bila kubughudhiwa ili pia waweze kuchangia katika pato la Taifa.