October 5, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Chalamila awashukia walioandaliwa kufanya vurugu

Na Esther Macha,Timesmajira Online, Mbeya

SERIKALI Mkoani Mbeya imesema, imepata taarifa ya kuwepo kwa vikundi vya vijana kupitia vyama vya upinzani ambao wameandaliwa kwa ajili ya kufanya vurugu katika vituo vya kupigia kura katika Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani utakaofanyika Oktoba 28 mwaka huu.

Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Albert Chalamila ametoa taarifa hiyo leo alipokutana na waandishi wa habari ofisini kwake na kuahidi Serikali haitovumilia na itawashughulikia ikiwa ni pamoja na watakaojihusisha kufanya maandamano, kulala barabarani na hatopenda kusikia mtu, watu kupoteza maisha wala kupata ulemavu kupitia uchaguzi wa mwaka huu.

“Kuna vyama vya siasa vimeandaa vijana 150 katika majimbo ya Rungwe na Mbeya Mjini kupita kwenye vituo vya kupigia kura na kufanya vurugu kwa lengo la kuleta machafuko na kuvuruga uchaguzi, niwaeleze tu kwamba, atakayefanya vurugu atalipwa kwa vurugu na atakayetenda mema atalipwa kwa mema yake, amesema Chalamila.

Aidha amewataka wananchi kujitokeza kupiga kura Oktoba 28 kwani ulinzi umeimarishwa na pindi watakapomaliza zoezi la kupiga kura waondoke kwenye vituo na kurejea majumbani mpaka Tume ya Uchaguzi itakapotangaza matokeo ya Urais, Ubunge na Udiwani.

Kuhusu vifaa vya kupigia kura, kiongozi huyo amesema kuwa, tayari vimefika na vipo katika hali ya ulinzi na usalama na hakuna dosari zitakazojitokeza kutokana na uhaba wa vifaa siku ya uchaguzi

Msimamizi msaidizi wa Uchaguzi Mkoa wa Mbeya, Mwajabu Abdalla amesema kuwa, Tume imejipanga katika kila kituo kuwa na vifaa vya kisasa vya maji tililika na sabuni kutokana na kuwepo na mwingiliano wa wapigakura na wageni kutoka nje nchi watakaofika mkoani hapa kwa ajili ya uchaguzi.