September 2, 2026

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Ilemela yatakiwa kusimamia mifumo ukusanyaji mapato 

Na Mwandishi Wetu,TimesMajira Online,Mwanza 

HALMASHAURI ya Manispaa imetakiwa kusimamia mifumo ya kukusanyaji  fedha hususani katika ngazi za vituo vya kutolea huduma ikiwa ni maelekezo ya Serikali kuwa makusanyo yote yafanyike kupitia mifumo ya kielektroniki.

Rai hiyo imetolewa na Katibu Tawala Msaidizi Usimamizi, Ufuatiliaji na Ukaguzi Kusirie Swai wakati wa uwasilishaji wa taarifa ya hesabu za mwisho za Halmashauri ya Manispaa ya Ilemela kwa mwaka wa fedha ulioishia  30 Juni,2026 iliyowasilishwa mbele ya Baraza la Madiwani na Mkurugenzi wa halmashauri  hiyo  Agosti 31,2026.

Amesema,ni jukumu la Mwekahazina kuhakikisha kila fedha inarudi vituoni kwa kuwasiliana na benki ili vituo viendelee kukusanya lengo ni kuhakikisha  mapato yanayokusanywa kwenye vituo hivyo  vya kutolea huduma yanahesabiwa katika Pato la Taifa ndio maana ya kuwekewa “control number”.

Pia  amesistiza juu ya suala la ukusanyaji wa mapato ya ndani ili kufanikisha utekelezaji wa majukumu  pia  kutozalisha madeni ya watumishi sambamba na ununuzi wa mashine za kusaini,(biometric machine),katika vituo vya kutolea huduma za afya ili kurahisisha masuala ya bima ya afya.

Ofisa Tawala wa Wilaya ya Ilemela akimwakilisha Katibu Tawala wa Wilaya hiyo Anna Mbao,amesistiza matumizi ya mifumo ya ukusanyaji wa mapato.

Kwa upande wake Mstahiki Meya wa Halmashauri Manispaa ya Ilemela Sarah Ng’hwani,amewataka Madiwani kutoa ushirikiano kwa wataalam sambamba na kusimamia vyema kata zao huku akiahidi kufanyia kazi na kusimamia utekelezaji wa maelekezo yaliyotolewa.

Akiwasilisha taarifa ya hesabu za mwisho za Halmashauri ya Manispaa ya Ilemela,Geofrey Temenao kwa niaba ya Mkurugenzi  wa halmashauri hiyo amesema,matokeo yaliyowasilishwa yanaonesha namna halmshauri ilivyokusanya na kutumia rasilimali zilizokuwa chini ya usimamizi wake katika kutekeleza majukumu yake ya  miradi na utoaji wa huduma kwa wananchi.