Na Mwandishi wetu,Timesmajira
Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Angela Kairuki, ameiagiza Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL) kuongeza kasi ya uunganishaji wa huduma ya intaneti ya mkongo wa nyuzi majumbani (Fiber to the Home – FTTH) ili kufikisha huduma hiyo katika nyumba milioni moja ifikapo Juni 2028.
Kairuki ametoa agizo hilo leo, Agosti 21, 2026, jijini Dar es Salaam, wakati akizindua rasmi awamu ya pili ya mradi wa “Fiber Mlangoni Kwako”, unaotekelezwa na TTCL kwa lengo la kuongeza upatikanaji wa intaneti yenye kasi, ubora na uhakika kwa wananchi, taasisi na wafanyabiashara Tanzania Bara na Zanzibar.
Amesema mradi huo ni sehemu ya jitihada za Serikali za kuimarisha uchumi wa kidijitali, kwa kuwa intaneti ya kasi inawawezesha wananchi kupata fursa za elimu, ajira, biashara, ubunifu na huduma mbalimbali za kijamii na kiuchumi.
“Fiber si waya tu unaofika nyumbani au ofisini, bali ni daraja muhimu linalomuunganisha mwananchi na fursa za uchumi wa kidijitali,” amesema Kairuki.
Kwa mujibu wa Kairuki, takwimu za Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) kwa robo mwaka iliyoishia Juni 2026 zinaonyesha kuwa usajili wa intaneti nchini ulifikia milioni 62.7, huku matumizi ya data yakifikia petabytes 1,041.
Hata hivyo, amesema watumiaji wa huduma ya fiber majumbani walikuwa 178,904 pekee, hali inayoonyesha bado kuna pengo kubwa kati ya mahitaji ya intaneti na upatikanaji wa huduma ya fiber kwa kaya.
Kairuki amesema awamu ya pili inalenga kuongeza wigo wa huduma hiyo hadi kufikia home passes 500,000, kabla ya kufikisha milioni moja ifikapo Juni 2028. Amesisitiza kuwa mafanikio ya mradi hayapaswi kupimwa kwa idadi ya nyumba ambazo fiber imepita pekee, bali pia kwa idadi ya wateja wanaounganishwa, ubora wa huduma, kasi halisi ya intaneti, muda wa kutatua hitilafu, gharama na kuridhika kwa wateja.

“Hatupaswi kuridhika na fiber kupita mbele ya nyumba ikiwa kaya haiwezi kujiunga. Hatupaswi kuridhika na usajili ikiwa huduma haitimizi ahadi ya kasi na uhakika,” amesema.
Ameitaka TTCL kupanua huduma hiyo katika maeneo yanayokua kwa kasi, vituo vya biashara, masoko, maeneo ya viwanda, shule, vyuo, vituo vya afya na ofisi za Serikali Tanzania Bara na Zanzibar.
Aidha, ameitaka kurahisisha taratibu za usajili, kupunguza muda wa kuunganisha huduma na kushirikiana na serikali za mitaa, waendelezaji wa makazi, wamiliki wa majengo na jumuiya za wafanyabiashara ili kuongeza idadi ya watumiaji.
Katika kuboresha huduma kwa wateja, Kairuki ameitaka TTCL kuimarisha ufuatiliaji wa mtandao, matengenezo ya kinga na urejeshaji wa huduma kwa haraka, pamoja na kuanzisha mifumo rahisi ya kupokea na kufuatilia malalamiko.
Amesema mteja hapaswi kulazimika kufuatilia mwenyewe tatizo aliloripoti, bali TTCL inapaswa kumjulisha hatua zilizofikiwa na kuhakikisha changamoto yake inatatuliwa kwa wakati.
Kairuki pia ameitaka TTCL kubuni vifurushi vinavyoweza kumudu kaya na makundi mbalimbali, wakiwemo wanafunzi, vijana, wafanyakazi, wavuvi, wachimbaji, wafanyabiashara wadogo na wa kati pamoja na taasisi, akisisitiza kuwa gharama za kuunganisha huduma, vifaa na vifurushi hazipaswi kuwa kikwazo.
Katika hatua nyingine, ameitaka TTCL kusimamia kwa karibu wakandarasi na wazabuni wanaotekeleza miradi hiyo ili kazi zikamilike kwa wakati, kwa ubora na kwa kuzingatia mikataba, huku kila shilingi inayowekezwa ikitoa thamani kwa shirika na Taifa.
Amesema Serikali inalenga kuona TTCL ikiwa na zaidi ya wateja milioni mbili hadi milioni tatu wanaotumia huduma za fiber majumbani ifikapo mwaka 2030.

Kwa upande wake, Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu, Abubakar Asenga, ameishauri Serikali kuongeza uwekezaji na bajeti kwa TTCL ili kuwezesha upanuzi zaidi wa huduma za intaneti kupitia mradi huo.
Asenga amesema Bunge kupitia Kamati hiyo limekuwa likisisitiza kwa miaka kadhaa umuhimu wa kuimarisha TTCL ili iweze kuwa chombo muhimu katika kufikisha huduma za mawasiliano kwa wananchi na kuongeza mapato ya Taifa.
Amesema ushauri wa Kamati wa kukabidhi TTCL jukumu la kusimamia shughuli hiyo umeanza kuonyesha matokeo, akieleza kuwa hadi mwaka wa fedha 2024/25, shirika hilo lilikusanya takribani Sh bilioni 100 kupitia kuunganisha wateja wapatao 280,000.
Kwa mujibu wa Asenga, mpango ni kufikisha mapato ya takribani Sh bilioni 400 ifikapo mwaka 2029 baada ya kuunganisha wateja milioni moja, huku idadi ya wateja milioni mbili ikiweza kulifikisha shirika kwenye mapato yanayokaribia Sh trilioni moja ifikapo mwaka 2030.
Naye Mkurugenzi Mkuu wa TTCL, Moremi Marwa, amesema awamu ya pili ya mradi huo ni sehemu ya utekelezaji wa mpango mkakati wa kibiashara wa miaka 10 wa shirika, unaoanzia mwaka 2025/26 hadi 2034/35.
Marwa amesema mpango huo unalenga kuboresha huduma, kuongeza idadi ya wateja na mapato, kuimarisha uendeshaji wa kielektroniki, uwajibikaji na matumizi ya teknolojia za kisasa.
Amesema TTCL imeanza kutumia teknolojia ya kisasa ya GPON inayowezesha kutoa intaneti yenye kasi kubwa, kuunganisha wateja wengi kwa wakati mmoja, kupunguza gharama za uendeshaji na kuboresha ubora wa huduma ikilinganishwa na teknolojia ya Point-to-Point.
Kwa mujibu wa Marwa, awamu ya kwanza ya mradi ilitekelezwa katika maeneo ya kimkakati ya Dar es Salaam, Arusha, Dodoma, Geita, Iringa, Mbeya, Mwanza na Unguja Zanzibar, ambapo takribani home pass 38,000 zilijengwa, huku mtandao uliokuwa umejengwa awali kwa teknolojia ya Point-to-Point ukifikisha maunganisho takribani 33,000.
Amesema kutokana na kuongezeka kwa mahitaji ya intaneti, TTCL imeanzisha awamu ya pili itakayopanua huduma hiyo katika mikoa yote ya Tanzania Bara na Zanzibar.
Amesema utekelezaji wa awamu ya pili ulianza Julai 2026 na jumla ya home pass 400,000 zinatarajiwa kujengwa katika awamu hiyo.
“Mpango huu utapelekea takribani maunganisho 750,000 kuwa yamejengwa kufikia Juni 2027, na mpango wa Shirika ni kufikia maunganisho takribani milioni moja ifikapo Juni 2028,” amesema Marwa.
Amesema utekelezaji wa mradi huo utaongeza matumizi ya teknolojia ya kidijitali na kuchangia utekelezaji wa malengo ya Serikali ya kujenga uchumi wa kidijitali nchini.

More Stories
Kurasini Port Extension kuanza kutumika Novemba
Makame awakalia kooni Ma-DC,utitiri vituo vya ukaguzi
Ujuzi wa Wezesha Binti wawasaidia vijana kujiajiri na kupata ajira