September 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

DC Mtanda amsimamisha kazi aliyefungia watoto chumba kimoja na Nguruwe

Na Israel Mwaisaka, TimesMajira Online Nkasi

MKUU wa Wilaya ya Nkasi mkoani Rukwa, Said Mtanda ameagiza kusimamishwa kazi mara moja kwa Afisa Mtendaji wa kijiji cha Matala, Revocatus Tinga kwa kosa la kuwakamata watoto wanaodaiwa kuwa watoro shuleni na kuwafungia chumba kimoja na Nguruwe.

Akizungumza na Wakazi wa kijiji cha Swahila, Mkuu huyo wa Wilaya amedai kuwa, baada ya kupata taarifa za tukio hilo, alimuagiza Mkurugenzi Mtendaji wa Wilaya kumsimamisha kazi na kumpeleka mtendaji mwingine.

Amesema kuwa, kitendo alichokifanya Afisa huyo hakikubaliki hivyo kwanza wamemsimamisha kazi na baada ya hapo atakabidhiwa kwenye vyombo vya dola kwa ajili ya uchunguzi na ikibainika kweli ametenda kosa hilo, ataadhibiwa kwa mujibu wa sheria na mamlaka yake ya nidhamu.

“Ni jambo lisilokubalika kwa mtendaji wa kijiji ambaye ni mlinzi wa amani katika kijiji na anafanya kitendo hicho sisi kama serikali ni lazima tuchukue hatua stahiki,” amesema kiongozi huyo.