March 7, 2026

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Kafiti ajiandaa kukabidhi bodaboda 100 Ilemela

*Ni kupitia programu ya Kafiti na Bodaboda 

*Kuwezesha vijana wa kata 19 kujiajiri na kuimarisha uchumi 

*Asema mpango huo ni sehemu ya utekelezaji wa ahadi zake za siku 100 za mwanzo

Judith Ferdinand,Mwanza

Katika kutekeleza ahadi zake za siku 100 za mwanzo, Mbunge wa Jimbo la Ilemela,Kafiti  Kafiti, amejipanga kutoa bodaboda 100 kwa vijana wa Kata 19 za Jimbo hilo, hatua ambayo ni fursa muhimu ya kuwawezesha kujiajiri na kujikwamua kiuchumi.

Pamoja na kukutana na vijana na wanawake ambao wamehitimu mafunzo ya stadi katika fani mbalimbali yaliotolewa na Chuo cha Ufundi Stadi(VETA) Mwanza,ili kuwezesha vikundi vyao kusajiliwa na kupata mikopo ya asilimia 10 ya halmashauri.

Kafiti amezungumza hayo Desemba 17,2025, mara baada ya kufungua mahafali ya mafunzo ya ufundi stadi kwa vijana na wanawake  wa Wilaya ya Ilemela na Nyamagana yaliofanyika kupitia programu ya Wanawake na Samia pamoja na mradi wa Vijana, Elimu, Malezi na Ajira(VEMA) unaotekelezwa  na shirika la Plan International  yaliofanyika VETA.

Ambapo amesema,yupo tayari kuona vijana wanainuka kwani anaamini wakiwasaidia wakaweza kujiajiri  itasaidia kujikwamua kiuchumi binafsi na taifa kwa ujumla.

Amesema wakati wa kampeni moja ya   ahadi ambayo aliahidi kuitekeleza ndani ya siku 100 za mwanzo za uongozi wake ni kutoa bodaboda 100 kwa vijana wa  kata 19 p jimboni Ilemela kwa maana kila kata itapata bodaboda 5.

“Programu hiyo inaitwa Kafiti na Bodaboda,na sasa hivi tunamalizia kuwasajili na Mungu akijalia Desemba 20,2025 tutakabidhi bodaboda hizo kwa  vijana.Nitahakikisha kila bodaboda jimboni Ilemela anapata leseni pamoja na elimu ya kuendesha chombo hicho kwani kundi hili  limeajiri vijana zaidi ya  10,000,”amesema Kafiti.

Pia amesema,wataendelea kuhakikisha vijana wenye elimu tofauti wanaweza kujikwamua kiuchumi ambapo kuna baadhi yao   kama Mbunge atawashika mkono katika eneo la kuajiriwa na wengi katika kujiajiri kwa kuwapa mafunzo na ujuzi huku  jambo kubwa atakalolifanya ni kuwapa mitaji pamoja na kuwezesha  wajasiriamali wadogo.

“Kupitia programu hizo za Wanawake na Samia na mradi wa VEMA,i nimeisha ongea na uongozi wa VETA,Desemba 29,2025 tutakutana hapa na wahitumu hao tukiwa na Maofisa Maendeleo  ya Jamii  wa Wilaya ya Ilemela ili kuweza kuwaunganisha katika vikundi,kuwasajili kutoa elimu ya namna ya kuingia katika mfumo  ili tuweze kuwapatia hiyo  mikopo ya asilimia 10 na kuweza kujiajiri,”amesema Kafiti.

Kwa upande wake  Mratibu wa Wanawake na Samia wa Wilaya ya Ilemela,Zuhura Salaam,amesema mafunzo hayo yalianza Septemba 2025 chini ya ufadhili wa Rais Samia Suluhu Hassan yakiwa na lengo la kusaidia wanawake kupata ujuzi wa fani mbalimbali nchini kupitia vyuo vya ufundi stadi(VETA).

Zuhura amesema,ambapo Mkoa wa Mwanza ulianza na wanawake 2214 kwa awamu mbili huku waliofanikiwa kuhitimu mafunzo hayo katika kozi 15 ni wanawake 1912,waliokatisha mafunzo ni 300  huku aliyefariki akiwa  mmoja.

“Awamu ya tatu ya mafunzo hayo inatanza Januari 2026 ikitarajia kushirikisha wanawake 515.Tunaomba tupate mikopo ya asilimia 10 kwani elimu tayari tumeisha pata,ofisi ya Wanawake na Samia kwa Mkoa wa Mwanza pamoja na kupata mitaji wezeshi kupitia sekta binafsi na Serikali,”amesema Zuhura.

Huku akibaisha changamoto zilizowakabili baadhi ya wanawake na kushindwa kuendelea na mafunzo ni pamoja na kuzuiliwa na wenza wao kwa sababu zao binafsi.