Na Agnes Alcardo, Timesmajira Online
KAMPUNI ya Bia Serengeti imezindua rasmi kinywaji kinachofahanika kama TZEE, kinywaji ambacho kipo katika mfumo wa ‘Gin’.
Kinywaji hiko kimezalishwa ndani ya viwanda vya SBL hapa nchini, huku TZEE ikielezwa kuwa ni ishara ya umoja na mafanikio ya kiuchumi wa ubunifu, ikiwakilishwa na kauli mbiu “TZEE ni SISI” kauli inayosisitiza kwamba kinywaji hiki ni cha Watanzania wote.
Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Bia ya Serengeti, Obinna Anyalebechi, amesema kuwa kuzinduliwa kwa TZEE ni hatua muhimu katika safari ya kampuni hiyo ya kuendeleza utamaduni wa vinywaji hapa Tanzania.
“TZEE imezaliwa kutokana na roho ya Kitanzania, imetengenezwa na Watanzania, kwa ajili ya Watanzania. Inawakilisha sisi kama taifa lenye thamani, ubunifu, na umoja. Uzinduzi huu si tu kuhusu bidhaa mpya, bali ni kusherehekea utambulisho wetu wa pamoja na fursa tunazoweza kuzipata tukiamini katika ubunifu wetu wenyewe,” amesema Obinna Anyalebechi.

Ameongeza kuwa mbali na ladha yake kuwa ya kipekee na ubunifu wa muonekano wake, TZEE ni jukwaa la kukuza uchumi na ubunifu wa Tanzania hasa kwa vijana wanaoibuka na kuendeleza utamaduni kupitia muziki, sanaa, mitindo, na ubunifu wa kidijitali.
“TZEE inasherehekea nguvu, ubunifu na fikra za kizazi kipya. Ni zaidi ya kinywaji ni alama ya ubunifu wa Kitanzania na nafasi ya kujieleza na kushirikiana. Kila mdundo, kila wazo, na kila tukio linalosheherekewa chini ya ‘TZEE ni SISI’ linaakisi vijana wa Kitanzania na nguvu ya ubunifu tunayoshikilia pamoja,” ameongeza Obinna Anyalebechi.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Masoko na Ubunifu wa SBL, Henry Esiaba, ameeleza kuwa TZEE ni zao la ubunifu wa ndani na kielelezo cha utamaduni unaoendelea kukua nchini Tanzania.
“TZEE ni chapa iliyogunduliwa kutokana na maarifa ya ndani na ushirikiano wa wabunifu wazalendo. Tulitaka kunasa miondoko, fahari, na utu wa Kitanzania ndani ya chupa, kitu kinachohisi kuwa chetu halisi. Kauli ‘TZEE ni SISI’ si maneno tu, ni wito wa umoja na sherehe ya utambulisho wetu,” amesema Henry.
Akaongeza kuwa TZEE inaashiria zama mpya za ubunifu unaoongozwa na watumiaji wa ndani, ambapo mawazo ya Kitanzania yanazalisha bidhaa zenye viwango vya kimataifa.

“Uundaji wa TZEE unaonyesha nguvu ya ubunifu wa ndani, unathibitisha kwamba tukiamini katika uwezo wetu, tunaweza kujenga chapa zinazochochea fahari na maendeleo. TZEE si kinywaji pekee bali ni harakati yenye mizizi ya uhalisia na ubora wa Kitanzania,”
ameongeza.
Kupitia TZEE, SBL inaendelea kupanua wigo wa ubunifu wake na kuimarisha nafasi yake kama kinara katika soko la vinywaji vikali nchini. Chapa hii ni sherehe ya uzalendo, umoja, na uwezeshaji wa uchumi na ubunifu uliobuniwa kwa ajili ya kizazi kinachoiona Tanzania si tu kama nchi, bali kama mwamko wa maendeleo na ubunifu.

More Stories
Bilioni 7 kuwainua vijana 308 sekta ya uvuvi
Clara:Miaka 50 ya Sabasaba fursa mpya za Biashara na Uwekezaji
Usajili wa Laini za Simu: Jilinde Dhidi ya Kutumiwa Vibaya kwa Utambulisho Wako