
Na Joyce Kasiki, TimesMajira Online – Arusha
KAMPUNI ya ZOLA inayojishughulisha na usambazaji wa mitambo ya umeme wa jua, imesema imejipanga kuunga mkono juhudi za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, katika kuhakikisha Tanzania inahamia kwenye matumizi ya nishati safi ifikapo mwaka 2030.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Arusha wakati wa maonesho ya Karibu-Kilifair 2025 Mwakilishi wa kampuni hiyo, Priscar Mbise, amesema ZOLA imeshiriki maonesho hayo kwa lengo la kuwafahamisha wananchi juu ya bidhaa zao za umeme wa jua, ambazo zimebuniwa kusaidia Watanzania wa kila hali ya kiuchumi kuachana na matumizi ya nishati chafu na kuchangia uhifadhi wa mazingira.
“Tunatoa huduma ya mitambo ya umeme wa jua inayopatikana kwa gharama nafuu kuanzia shilingi 600 kwa siku, jambo linalomuwezesha kila Mtanzania kumudu kupata nishati safi. Pia tunatoa dhamana (warranty) ya hadi miaka sita kwa mitambo hii,” alisema Mbise.
Mbise alieleza kuwa kampuni hiyo ambayo Makao Makuu yake yapo jijini Arusha , pia inafunga mitambo mikubwa ya umeme wa jua kwenye taasisi kama hospitali, shule, hoteli na viwanda. Alitoa mfano wa hospitali ya Mount Meru jijini Arusha, ambako tayari wameshafunga mitambo katika wodi ya mama na mtoto.
“Tunayo mitambo mikubwa kuanzia 5KVA hadi 25KVA inayoweza kutumika katika maeneo makubwa kama hospitali na viwanda, na tunaiuza kwa bei nafuu kabisa ili kila taasisi iweze kuhamia kwenye nishati safi,” aliongeza.
Mbise amesema nishati ya jua ni salama, rafiki kwa mazingira na ya uhakika hata kwa wale wasiounganishwa kwenye gridi ya Taifa, kwani inaweza kuendesha vifaa vyote vya umeme bila usumbufu.
“Kampuni ya ZOLA inatoa huduma kwa sekta mbalimbali kama elimu, afya, utalii na wananchi wa kawaida. Tunaamini juhudi zetu zinaenda sambamba na dira ya Rais Samia ya kuhakikisha Tanzania inatumia nishati safi ifikapo mwaka 2030,” amesema Mbise
Amewataka Watanzania kuendelea kujifunza kuhusu teknolojia hiyo ZOLA na kuitumia kwa manufaa yao binafsi na ya Taifa kwa ujumla.
More Stories
Kiongozi wa Mwenge awataka RUWASA kukamilisha mradi wa maji kwa wakati Kilindi
Balozi Nchimbi aongoza waombolezaji kumuaga Mzee Mongella
Ahukumiwa kunyongwa hadi kufa kwa kumuua mama yake mzazi