March 7, 2026

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Yas yaja na ‘Anzia Ulipo’ kuhamasisha watanzania kusimamia ndoto zao

Na Mwandishi Wetu, Timesmajira Online

KAMPUNI ya Mawasiliano hapa nchini, inayoongoza kwenye masuala ya kidijitali Yas, imezindua rasmi Kampeni kabambe ya ‘Anzia Ulipo’ yenye lengo la kuwahamasisha watanzania kutimiza ndoto zao kwa kutumia kile kidogo walichonacho.

Kampeni hiyo inawahasa watanzania kuanza sasa na kuacha visingizio ya kutokuwa tayari kufanya jambo fulani.

Aidha, Kampeni hiyo iliyozinduliwa jijini Dar es Salaam inaonyesha dhamira ya Yas kuwawezesha Watanzania kustawi katika ulimwengu wa kidijitali unaokua kwa kasi.

Mbali na hivyo, pia Kampeni hiyo inalenga kuleta fursa zisizo na mipaka kupitia teknolojia, kukuza ubunifu, na kuhakikisha ndoto za watanzania zinatimia.

Akizungumza katika hafla ya uzinduzi huo, Afisa Mtendaji Mkuu wa Yas, Pierre Canton Bacara, amesema kuwa ‘Anzia Ulipo’ si kampeni ya kawaida bali ni harakati ya kitaifa.

“Tanzania ni nchi ya watu wenye ndoto kubwa, wabunifu, wachakarikaji na watu wenye fikra mpya,” alisema Bacara. “Tunaamini kuwa kungoja muda muafaka si suluhisho la kuzifikia ndoto tena.

“Tayari sisi kama Yas tumewekeza pakubwa katika miundombinu imara ya kidijitali nchini kote – ambayo ndio msingi wa maendeleo ya elimu, afya, kilimo, biashara mtandaoni na ujasiriamali.

“Uwekezaji huu ndio unaomwezesha mwalimu kule Mtwara kufundisha mtandaoni, mkulima Mbeya kujua bei za soko papo kwa papo, na mjasiriamali wa Arusha kuwafikia wateja duniani kote.

”Kwa mujibu wa Sensa ya Taifa ya 2022, zaidi ya asilimia 34.5 ya Watanzania wana umri kati ya miaka 15 hadi 35, kundi kubwa la vijana ambalo mara nyingi hujihisi kukwama kutokana na ukosefu wa rasilimali au fursa,” amesema.

Katika uzinduzi huo, vijana mbalimbali waliotoa ushuhuda walionesha namna teknolojia inavyoweza kubadilisha maisha inapounganishwa na juhudi na ubunifu.Kwa upande wake, Isack Nchunda,

Afisa Mkuu wa Biashara wa Yas, alisisitiza umuhimu wa kuchukua hatua.“Kila safari ya mafanikio huanza kwa uamuzi wa kuanza pale ulipo, na kutumia kile ulicho nacho. Hii ndiyo azma Kampeni hii ya Anzia Ulipo.

Msanii wa muziki wa Bongo fleva, Isaya Michael Mtambo maarufu ‘Chino Kidd’ (wa pili kutoka kushoto) akitumbuiza katika hafla ya uzinduzi wa Kampeni ya “Anzia Ulipo” uliofanyika Juni 4, 2025, jijini Dar es Salaam. Kampeni hiyo inalenga kuwatia moyo Watanzania kuanza kutimiza ndoto zao kwa kutumia fursa na rasilimali walizonazo, badala ya kusubiri mazingira kuwa kamilifu.

“Hatuuzi tu teknolojia, tunauza imani ya kuwa kila Mtanzania, popote alipo na chochote alicho nacho, anaweza kubadilisha wazo kuwa matokeo, na ndoto kuwa mafanikio. Kampeni hii ni mwito wa kweli kwa kila Mtanzania mwenye ndoto, kipaji au wazo kuanza sasa, na kutumia miundombinu tuliyojenga pamoja na huduma na bidhaa zetu zilizobuniwa mahsusi kwa ajili ya kufungua fursa zilizomo ndani ya uwezo wao.

”Kupitia kampeni hii ya Anzia Ulipo, Yas inaendelea kujidhihirisha kuwa mshirika wa kweli wa maendeleo, ikitoa huduma bora zaidi za mtandao wa 4G na 5G pamoja na suluhisho za kidijitali zinazojibu mahitaji halisi ya vijana wa leo,” amesema.