October 6, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Yanga yatinga nusu fainali FA Cup

Na Hamisi Miraji

MABINGWA wa kihistoria katika Ligi Kuu Tanzania Bara Yanga, jana, wamefanikiwa kutings nusu fainali ya Kombe la Shirikisho baada ya kuifunga Kagera Sugar goli 2-1, katika mchezo wa robo fainali uliofanyika Uwanja wa Taifa Dar es Salaam.

Mchezo huo ambao ulikuwa wa ushindani mkubwa huku Kagera Sugar wakiutawala mchezo kwa dakika zote, licha ya kukubali kichapo.

Kagera Sugar ndio walikuwa wa kwanza kuzifumania nyavu za Yanga katika dakika ya 19 kupitia kwa kiungo wake Awesu Awesu, baada ya kupata pasi kutoka kwa Yusufu Muhiru.

Hata hivyo, Yanga walijipanga na kusawazisha goli dakika ya 51 kupitia kwa mshambuliaji wake David Molinga.

Yanga walifanikiwa kupata goli la pili na la ushindi kwa mkwaju wa penalti uliofungwa na Deus Kaseke baada ya Mrisho Ngassa kuchezewa vibaya kwenye eneo la hatari na beki wa Kagera Sugar Juma Nyosso.

Dakika ya 77 mwamuzi amempa kadi nyekundu mfungaji wa Kagera Sugar Awesu Awesu licha ya kufanyiwa faulo nje ya 18.

Kwa matokeo hayo Yanga wanasubiri mshindi wa leo kati ya Azam FC na Simba ili kucheza mchezo wa nusu fainali.