October 5, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Yanga ya Kaze yawageukia Biashara United

Na Judith Ferdinand, TimesMajira Online, Mwanza

BAADA ya kocha mkuu wa klabu ya Yanga, Cedric Kaze kutoridhishwa na kile walichoonesha wachezaji wake katika mchezo wao uliopita dhidi ya KMC ambao walipata ushindi wa goli 2-1, ameona hakuna haja ya kupumzika baada ya jana kikosi hicho kueendelea na mazoezi kujiandaa na mchezo wao ujao wa Ligi Kuu Tanzania Bara (VPL) dhidi ya Biashara United ya Mara utakaochezwa Oktoba 30.

Katika mchezo huo, licha ya KMC kupata goli la kuongoza dakika ya 27 lililofungwa na Hassan Kabunda Yanga walisawazisha dakika ya 41 kupitia kwa Tuisila Kisinda lakini mshambuliaji Waziri Junior aliifungia Yanga goli la ushindi dakika ya 61.

Baada ya mchezo huo, Kaze alisema kuwa, bado ana kazi kubwa ya kukiboresha kikosi chake kwani kilishindwa kuhimili presha ya mchezo huo jambo lililofanya kushindwa kuwa makini.

Lakini pia kocha huyo aliweka wazi kuwa, ugumu wa mchezo huo pia uliwafanya wachezaji wake kushindwa kucheza vizuri kwenye mfumo ambao waliingia nao na kushindwa kufanya kile walichokitarajia.

Amesema, kabla ya kuruhusu goli, vijana wake walijaribu kucheza vizuri na kusukuma mashambulizi lakini kipindi cha pili ndio hakikuwa kizuri kwani walionesha kile ambacho hawakukitarajia licha ya kufanya mabadiliko ya baadhi ya wachezaji.

Katika mchezo huo, kikosi cha Yanga kilikuwa na mabadiliko ya baadhi ya wachezaji ambao hawakuanza katika mchezo wao uliopita dhidi ya Polisi Tanzania ambao nao walishinda goli 1-0.

Kaze amewaanzisha Michael Sarpong, Waziri Junior pamoja na Deus Kaseke lakini akiendelea kuiamini safu yake ya ulinzi golini akiendelea kusimama Metacha Mnata aliyesaidiwa na Kibwana Shomary, Yassin Mustapha, Lamine Moro na Bakari Mwamnyeto.

Sababu hizo ndizo zinazotajwa kumfanya kocha huyo, kusaka haraka ubora wa kikoshi chake kabla ya kukutana na Biashara United ambao wametoka kumfunga Polisi Tanzaniagoli 1-0 katika uwanja wake wa nyumbani wa Ushirika Moshi.

Ushindi huo umewanya kukaa nyuma ya Yanga katika msimamo wa Ligi wakiwa wamefikisha pointi 16 hivyo wanaamini wakishinda mchezo huo watawafikia kwa pointi.

Kaze ambaye ameiongoza Yanga katika mechi zote mbili ambazo amevuna alama sita, amesema bado ana kazi kubwa na kukiweka sawa kikosi chake ili kuhakikisha wabachukua alama tatu nyingine katika mchezo huo dhidi ya Biashara United.