May 2, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Wizara ya Elimu kusimamia utoaji elimu masuala ya fedha

Na Jackline Martin, TimesMajira Online

WIZARA ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
imeahidi kusimamia na kutekeleza ipasavyo utolewaji wa elimu ya masuala ya fedha kwa wanafunzi wa elimu ya juu ili taifa liweze kuwa na wataalam bobezi wa masuala ya kifedha.

Kauli hiyo imetolewa juzi Jijini Dar es
Salaam na Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Omary Kipanga wakati akifungua warsha ya siku tatu kwa viongozi wa vyuo mbalimbali nchini ili kujadili mitaala ya elimu ya fedha kwa wanafunzi wa elimu ya juu huku
ukiratibiwa na Benki Kuu ya Tanzania (BoT).

Alisema suala la elimu ya fedha kwa jamii ni muhimu kwa maendeleo ya nchi hivyo ni vyema elimu hiyo ikafika kwa jamii Ili watanzania waweze Kupata elimu ya masuala ya fedha.

Aidha Naibu Waziri Kipanga alisema serikali ya awamu ya sita imedhamiria kujenga uelewa wa masuala ya fedha kwa jamii.

“Wizara tutahakikisha elimu ya fedha
inafundishwa katika mfumo wa elimu nchini hivyo twende kwa haraka kuhakikisha vijana ambao ni sehemu ya jamii nchini wanakuwa na uelewa wa masuala ya fedha hivyo natarajia
wakuu wa vyuo mtabeba uelewa huo muhimu kwa vyuo vyetu nchini,” alisema Kipanga.

Pamoja na hayo alisema kuwa BoT,
itaendelea kusimama na vyuo na taasisi za
elimu na Wizara ya Elimu katika kuhakikisha dhana ya elimu hiyo inakuwa endelevu na inafundishwa katika ngazi za jamii hata katika elimu zisizo rasmi.

Hata hivyo ameviagiza vyuo vikuu kushirikiana na BoT kufanya tathmini ya utekelezaji wa mpango huo ili kuboresha mbinu na nyenzo za kufikisha ujumbe huo kwa jamii.

“Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
ipatiwe taarifa ya tathmnini mtakazofanya ili itusaidie katika kufanya maamuzi, serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Dk. Samia Suluhu Hassan imedhamiria kujenga uelewa wa masuala ya fedha kwa jamii,” alisema.

Kwa upande wake Naibu Gavana Benki
Kuu ya Tanzania Bi. Sauda Msemo alibainisha kuwa lengo la kutoa elimu ya fedha kwa Vijana wa kitanzania wanaosoma elimu ya juu ni kuwawezesha kupata ujuzi na uzoefu wa matumizi ya fedha.

Alisema takwimu ya Sensa ya Watu na
Makazi mwaka 2022 inaonesha takribani
watu asilimia 34.5 ni vijana walio na umri kati ya miaka 15-35 hivyo ili kuleta tija na ufanisi katika masuala ya uchumi ujuzi na uzoefu wa masuala ya fedha ni moja ya sifa muhimu kufikia azma hiyo.

Ameeleza kuwa elimu ya fedha kwa
Watanzania kutachochea maendeleo kwa
kuongeza utumiaji rasmi wa huduma za fedha na kuwawezesha watu wengi kuwa na uwezo wa kufanya maamuzi sahihi ya kifedha na kuendesha shughuli zao kwa ufanisi kukuza uchumi kwa ujumla.

Sauda mesema elimu kwa vijana wa vyuo
vikuu itawasaidia kuweka akiba, kupanga
bajeti na kufanya uamuzi wa masuala ya
fedha kwa kuzingatia viashiria hatarishi na
kuelewa taasisi mbalimbali zinazotoa huduma za fedha ili kufanya maamuzi sahihi ya fedha ili waitawale.

” Tunatarajia kujenga ‘displine’ ya fedha
kupitia elimu ya fedha kwani watakuwa
na uwezo wa kutawala fedha sio fedha
kuwatawala vijana hao,” alisema.

Pia alisema BoT kwa kushirikiana na wadau wengine wa Baraza la Huduma Jumuishi za Fedha, imetoa muongozo na mtaala wa elimu ya fedha kwa wakufunzi ambao utatumika na taasisi za elimu ya juu kwa kuwafundisha watoa huduma za elimu ya fedha kuwafikia wananchi
wote walio nje mfumo wa elimu.

“Tayari tumeingia makubaliano na baadhi ya taasisi zaa elimu katika mtaala huo wa kufunzi wa fedha na tulioingia nao makubaliano ni Chuo Kikuu cha Iringa, Zanzibar, Chuo Kikuu cha Usimamizi wa Fedha(IFM) na Chuo cha Benki Kuu ya Tanzania ,” alisema.

Katika warsha hiyo imebainishwa kuwa
elimu ya fedha inapaswa kumfikia kila mmoja ili aweze kuwa na nidhamu katika matumizi ya pesa lakini kuepuka kuingia kwenye sitofahamu ambayo inawakuta wengi hasa wanapokwenda kwenye taasisi za mikopo.