September 28, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Wazazi,walezi waombwa kutenga muda wa kuzungumza na watoto wao

Na Mwandishi wetu , Timesmajira

KATIKA kuelekea siku ya Kimataifa ya Mtoto wa Afrika inayoadhimishwa kila ifikapo Juni 16 wazazi na walezi wameombwa kutenga muda wa kuzungumza na watoto ili kujua Changamoto mbalimbali ambazo wanakumbana nazo .

Pia wameombwa kuepuka migogoro ya kifamilia ili kumlinda mtoto dhidi ya msongo wa mawazo inayopelekea baadhi ya watoto kujidhuru au kubadilika kitabia.

Akizungumza na waandishi wa habari katika Kituo cha Utamaduni cha Ubalozi wa Ufaransa nchini ‘Alliance Francaise’ kuelekea Maadhimisho hayo, Mwanaharakati wa haki za watoto Adela Alex amesema ni muhimu wazazi kutenga muda wa kuzungumza na watoto hii itawasaidia kubaini ni Chagamoto gani wamekuwa wakikabiliana nazo.

“Wazazi na walezi wamekuwa hawana mda na ukaribu wa kutosha wa kuzungumza na watoto wao … kutokana na wengi wao kuwa bize..hata pale wanapokuwa nyumbani watoto wanapowafata udai wako bize”amesema Adela.

Kuhusu migogoro katika familia Adela amesema Watoto wengi wanaumia wanapowaona wazazi wao wakiwa katika migogoro ya familia na awalezi jambo ambalo Hali hiyo ujijenga katika fikra zao na badae kupelekea kumpa msongo wa mawazo .

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya Maadhimisho hayo kutoka taasisi ya All Together in Dignity Tanzania (ATD) ,Agatha Makombe amehimiza wazazi na walezi kuwalea watoto katika misingi na maadili ya kitanzania na kutenga muda wa kuzungumza nao ili kufahamu changamoto wanazopitia.

Amesema hatua hiyo itasaidia kuwaepusha watoto na msongo wa mawazo unaowasababishia kuchukua maamuzi magumu kutokana na vitendo vya kikatili katika familia na jamii.

Akizungumzia kuhusu Maadhimisho hayo amesema Shirika limeandaa maadhimisho hayo amesema ni sehemu ya njia ya kupaza sauti na kuonesha utetezi wao kwa watoto.

” Tunafanya kazi na watoto wanaoishi kwenye mazingira ya umasikini uliokithiri na mwaka huu tumejikita katika elimu jumuishi kwa mtoto ambayo lazima izingatie maarifa, maadili na stadi za kazi na kwa upande wa wazazi na jamii wanatakiwa kushirikiana bega kwa bega na watoto kwa kuhakikisha mustakabali wao unakuwa mzuri.” amesema

Aidha amesema kauli mbiu ya mwaka huu ya ‘Elimu Jumuishi kwa Watoto Kuzingatie Ujuzi, Maadili na Stadi za Kazi; Wajibu wa Wazazi na Jamii Katika Kumsaidia Mtoto katika Kufikia Malengo yake kwa Maendeleo ya Baadaye.

Agatha amesema, Taasisi hiyo imejikita katika nyenzo ya elimu kwa kuwa humpatia mtoto mwanga, ujuzi na maarifa ya kuweza kutambua alipo na namna ya kupambana dhidi ya hali iliyopo kwa ubora wa baadaye.”ATD imekuwa ikifanya kazi ya utetezi katika maeneo mbalimbali kwa watoto wanaoishi katika umasikini uliopitiliza pamoja na matatizo mbalimbali ikiwemo magonjwa adimu kwa kuhakikisha wanapata elimu ili mtoto apate haki msingi ya elimu ili kuweza kumkomboa kifikra”amesema

Naye Mratibu wa kitengo cha Maendeleo ya Jamii anayehusika na Dawati la mtoto kutoka Manispaa ya Kinondoni Clara Urasa amesema, katika kumwendeleza mtoto dawati hilo humsaidia mtoto katika shughuli za shule na jamii kwa ustawi wao kwa kuhakikisha analindwa katika kufikia ndoto zao.

Amesema, kupitia mabaraza ya watoto, majukwaa na klabu za watoto wamekuwa wakitoa elimu mbalimbali kuhusiana ma malezi, utu wema, uongozi na maadili ili kuwalinda dhidi ya mabadiliko ya teknolojia katika makuzi yao.

Aidha amesema wanazingatia muongozo wa Taifa unatoa mweleko wa namna ya kuwafundisha watoto dhidi ya mmomonyoko wa maadili na kumfanya mtoto aweze kusimama katika haki zake.