October 8, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Watumishi wa umma watakiwa kutimiza wajibu

Na Agnes Alcardo, Timesmajira Online. Tanga

KATIBU Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, amewataka watumishi wa umma nchini kutimiza na kutekeleza majukumu yao, hususani katika usimamizi wa miradi ya maendeleo ili kuhakikisha inakamilika kwa wakati.

Nchimbi, ameyasema hayo Juni 7,2024 wakati akizungumza kwenye mkutano wa hadhara na wananchi wa Wilaya ya Korogwe mkoani Tanga, akiwa kwenye muendelezo wa ziara yake ya mikoa mitano, yenye lengo la kuangalia uhai wa chama, utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi mwaka 2020/2025.

Katika mkutano huo wa hadhara uliofanyika kwenye uwanja wa Manundu, Mjumbe wa Halmashauri Kuu CCM Taifa Mkoa wa Tanga, Mohammed Ratco, ameomba kuchukuliwa hatua kwa watendaji wazembe waliokwamisha miradi ya maendeleo wilayani humo.

“Kumekuwa na uzembe wa watumishi wachache kutotimiza majukumu yao hali inayosababisha ucheleweshwaji wa maendeleo katika Wilaya yetu,”amesema Ratco.

Kwa upande wake Katibu wa NEC, Itikadi, Uenezi na Mafunzo CCM Taifa, CPA Amos Makalla, ameendelea kuwasisitizia wananchi juu ya kuendelea kukiamini chama hicho na kumuunga mkono Rais Dkt. Samia kwa kumpatia kura za kisindo katika chaguzi zijazo.

Aidha katika mkutano huo Chama cha Mapinduzi (CCM), kimepokea wanachama wapya zaidi ya 200 kutoka vyama vya upinzani.