September 21, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Watu tisa wafariki kwa ajali,Mbeya

Na Esther Macha, Timesmajira Online,Mbeya

WATU tisa wamefariki huku wengine 18, wakijeruhiwa jijini Mbeya, baada ya basi la abiria la kampuni ya Shari line lenye namba T .896 DHK aina ya Yutong, kuacha njia na kugonga gema kisha kuanguka.Ambapo basi hilo lilikua likitokea mkoani Rukwa kuelekea Ubaruku wilayani Mbarali.

Akizungumza na waandishi wa habari Septemba 4,2024 Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya, Benjamin Kuzaga amesema kuwa tukio hilo limetokea Septemba 3 mwaka huu, majira ya saa 1 na dakika 10 jioni,kijiji cha Itamboleo Kata ya Chimala wilaya ya Mbarali mkoani Mbeya.

Kuzaga amesema kuwa,basi hilo lilikuwa likiendeshwa na dereva Afred Mwidunda (50) mkazi wa Ubaruku wilayani Mbarali.Ambapo ameeleza kuwa kati ya watu tisa waliofariki kati yao wanaume sita,watoto wawili na waliobaki wanawake ni (3)ambao wote bado hawajatambulika .

Aidha Kamanda Kuzaga amesema kuwa katika tukio hilo watu 18 walijeruhiwa kati yao wanaume 05, wanawake 13 na watoto 02 wa kiume na wa kike.

Kamanda Kuzaga amesema chanzo cha ajali hiyo ni uzembe wa dereva wa basi hilo kushindwa kulimudu gari hilo kwenye kona kali,hivyo kuacha barabara na kutumbukia korongoni na kugonga gema.Hata hivyo dereva wa basi hilo anaendelea kupatiwa matibabu katika hospitali ya Misheni Chimala akiwa chini ya ulinzi wa Jeshi la Polisi.

Kuzaga amesema miili ya marehemu imehifadhiwa hospitali ya Misheni Chimala.Huku majeruhi wakipatiwa matibabu hospitali ya Rufaa Kanda ya Mbeya na wengine hospitali ya Misheni Chimala.

Aidha jeshi hilo,limetoa wito kwa madereva kuwa makini na kuzingatia sheria, alama na michoro ya usalama barabarani ili kuepuka ajali zinazoweza kuepukika.

Akizungumzia tukio hilo la ajali Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbarali,Twalibu Lubandamo amesema kuwa tukio limetokea jana na miili na majeruhi wapo hospitali ya misheni Chimala.