September 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

‘Wapeni watoto fursa kushiriki mafunzo ya ushairi’

Na Mwanandishi Wetu,TimesMajira Online. Kisarawe

WAKATI Siku ya Ushairi wa Watoto (WoChiPoDa) ikiadhimishwa duniani kote wazazi, walezi na walimu nchini wametakiwa kuwapa fursa watoto wao ya kushiriki katika mafunzo na matamasha ya uandishi wa ushairi na usomaji vitabu, ili kuwajengea uwezo wa kuandika maandiko mbalimbali kulingana na mazingira wanayoishi kwani kufanya hivyo, kutasaidia kuibua na kuendeleza vipaji vyao katika kuliletea taifa maendeleo kwa siku za baadaye.

Hayo yamesemwa na Mratibu wa Siku ya Ushairi Mkoa wa Pwani, Rehema Kawambwa alipokua akizungumza katika maadhimisho ya Siku ya Ushairi wa Watoto yanayofanyika kila Jumamosi ya kwanza ya Oktoba ambayo mwaka huu yalifanyika katika Shule ya Msingi Kiluvya ‘B’ Kisarawe mkoani Pwani.

Rehema amesema ili kujenga uelewa kwa watoto kulingana na mazingira wanayoishi ni wazi kuwa ipo haja ya kila mzazi, kutambua kuwa watoto wana haki ya kushiriki katika matamasha kama hayo, ambayo yatawajengea uwezo wa kuwa waandishi wa ushairi na insha na vitabu mbalimbali vya hadithi na hatimaye kuwa sehemu muhimu ya kuielimisha jamii ya Watanzania.

Amesema kazi ya uandishi ni kazi kama kazi nyingine, hivyo endapo mtoto ataandaliwa vizuri na kuwa mwandishi mzuri si tu atakua sehemu ya kuwaelimisha wengine, lakini pia ujuzi na kipaji alichonacho kitamsaidia kujiingizia kipato kama ilivyo kwa waandishi wengine wenye majina makubwa duniani.