September 30, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Wanawake Singida waazimia kumchagua Magufuli

Na Mwandishi Wetu,TimesMajira Online. Singida

WANAWAKE Mkoa wa Singida wamesema wanamuunga mkono mgombea Urais wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dkt. John Magufuli katika Uchaguzi Mkuu unaotarajia kufanyika Oktoba 28 mwaka huu kutokana na mambo makubwa mazuri aliyoyafanya kwa kipindi cha miaka mitano iliyopita.

Akiwasilisha tamko hilo juzi kwenye kikao cha wanawake cha kutoa tamko hilo kilichofanyika katika Ukumbi wa Roman Catholic, Leonia Kiria kwa niaba ya wanawake hao mbele ya mgeni rasmi Aisharose Mattembe, mgombea Ubunge Viti Maalumu mkoani hapa kwa tiketi ya CCM, amesema kwa umoja wao kutoka katika makundi mbalimbali ya wanawake wameamua kumchagua Dkt. Magufuli.

Amesema baada ya kukaa na kutafakari kwa kina, wameamua kutoa tamko hilo kuwa katika uchaguzi huo watamchagua mgombea Urais wa CCM, Wabunge na Madiwani.

Leonia amesema wao kama wanawake, wapo ambao ni wajane hawana uwezo wa kuwalipia ada watoto wao lakini, Magufuli amewapunguzia mizigo hata waliokosa tumaini la kusomesha, kupitia elimu bila malipo watoto wao wanasoma bila usumbufu katika miundombinu ya barabara, hivyo kuwarahisishia kufanya biashara kila kona kwani barabara zinapitika.

Amesema wanalaani sera za baadhi ya wagombea wa vyama vya siasa zenye lengo la kuharibu utamaduni wa Watanzania, hivyo wao kama wanawake wanalaani sera hizo na hawatakubali kuona utamaduni wa Watanzania, unaharibiwa kwani atakayeathirika zaidi ni mwanamke huku akikemea kampeni zenye lengo la kuleta fujo zitakazo hatarisha amani.