September 20, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Wananchi wahamasishwa kufanya utalii wa ndani

Na Hadija Bagasha, Timesmajira Online, Morogoro

MKUU wa Wilaya ya Morogoro Mussa Kilakala, ameihamasisha jamii kujenga utamaduni wa kufanya utalii wa ndani na kutembelea vivutio vilivyopo, ikiwemo kivutio cha utalii cha Maji Moto kilichopo Kata ya Kisaki, kijiji cha Kisakimaji moto Wilayani Morogoro.

Kilakala ametoa rai hiyo, Septemba 19,2024,mara baada ya kutembelea cha Kisakimaji, na kujionea kivutio cha chemichemi inayotoa maji ya moto muda wote bila kikomo wala kupoa kwa maji hayo hata ikinyesha mvua.

“Mwenyezi Mungu ametubariki katika maeneo yetu, tunayo chemichemi ya maji moto, muda na wakati wote iwe kipindi cha jua au mvua maji yanakuwa ya moto, hususani majira ya asubuhi maji haya yanatoka mvuke kabisa karibu wilayani kwetu katika Kijiji hiki mjionee maajabu haya makubwa,” amehimiza DC. Kilakala.

Naye Ofisa Maliasili Wilaya ya Morogoro, Wahida Beleko, amesema chemichemi za maji moto zipo pia katika baadhi ya hifadhi nchini, lakini zinatofautiana kulingana na kiwango cha joto kilichopo.

“Chemichemi hizi zipo maeneo mengi, yapo hifadhi ya Taifa ya Mwalimu Nyerere, hata Ziwa Manyara yapo lakini ya kwetu kidogo ni tofauti,joto lake ni kali sana hasa majira ya asubuhi,”ameeleza na kuongeza:

“Cha ajabu hata mvua ikinyesha tunatarajia kuwa yatapozwa kutokana na maji ya baridi, lakini ndiyo yanakuwa yamoto zaidi, na maji haya kitaalamu yanatibu magonjwa ya ngozi,”.