September 23, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Wananchi wafurika uwanja wa majimaji kumsikiliza Rais Samia

Na Mwandishi wetu, Timesmajira

Katika hali ya hamasa kubwa, umati mkubwa wa wananchi wa Mji wa Songea umejitokeza kwa wingi kwenye Uwanja wa Majimaji, kumshuhudia na kumsikiliza Rais na Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dkt. Samia Suluhu Hassan, tarehe 23 Septemba 2024 katika kilele cha Tamasha la Tatu la Kitaifa la Utamaduni, lililoandaliwa na Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo, mkoani Ruvuma.

Rais Dkt. Samia ni mgeni rasmi wa tamasha hilo, lililojikita katika kuonesha na kusherehekea utajiri wa urithi wa kitamaduni wa Tanzania.

Kabla ya hotuba yake, Rais Samia alipata fursa ya kutembelea mabanda ya maonesho ya utamaduni, ambapo alijionea kazi mbalimbali za sanaa na utamaduni, na hata kushiriki kucheza mchezo wa bao, jambo lililowafurahisha wananchi na wasanii waliokuwepo.

Shughuli hiyo inaendelea kwa shamrashamra, huku wananchi wakionesha shauku na furaha kubwa kwa ziara ya Rais katika eneo hilo, likiwa na umuhimu mkubwa kwa historia na utamaduni wa taifa.