Na Mwandishi Wetu, Timesmajira Online
Zaidi ya wananchi 4,000, wilayani Bagamoyo mkoani Pwani,wamepatiwa matibabu ya macho bure kupitia kambi maalum iliyoandaliwa na kampuni ya Mawasiliano Yas kwa kushirikiana na Khoja Shia Ithnasheri Charitable Eye Centre (KSI) pamoja na Bilal Muslim Mission na Beta Trust.
Huduma zilizotolewa katika kambi hiyo ni pamoja na upasuaji wa mtoto wa jicho, usambazaji wa dawa, miwani ya bure na ushauri wa kitaalamu kutoka kwa madaktari bingwa wa macho.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa kambi hiyo, Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo, Shaibu Ndemanga, ameipongeza Yas na washirika wake kwa mchango huo kwa jamii.
“Afya njema ni msingi wa maendeleo ya kijamii. Huduma hizi za macho siyo tu zinarejesha uwezo wa kuona, bali pia zinawawezesha wananchi kushiriki kikamilifu katika shughuli za kijamii na kiuchumi .Tunaishukuru Yas na washirika wao kwa kugusa maisha ya wakazi wa Bagamoyo kwa vitendo,”amesema Ndemanga.
Kwa upande wake, Meneja wa Yas Kanda ya Pwani Kusini, Godbless Massawe,amesema hatua hiyo ni sehemu ya dhamira ya kampuni kuwekeza katika ustawi na maendeleo ya Watanzania nje ya biashara.
“Tunatambua kuwa mawasiliano hayatokuwa na msingi endapo wananchi hawana afya bora. Kupitia kambi hii tunahakikisha wakazi zaidi ya 4,000 wa Bagamoyo wanapata upasuaji, dawa na miwani bure,”amesema Massawe na kuongeza:
“Kwa mwaka huu pekee, Yas imefanikiwa kuwafikia Watanzania zaidi ya 25,000 nchini kupitia kambi za aina hii katika mikoa mbalimbali,”.

Naye Dkt. Ashraf Mlanzi kutoka Taasisi ya Bilal Muslim Mission,iliyoongoza zoezi zima la upimaji macho, amesema kambi hiyo imeleta faraja kwa wakazi wengi waliokuwa wakisumbuliwa na matatizo ya macho kwa muda mrefu.
“Magonjwa ya macho, hususani mtoto wa jicho, yamekuwa chanzo kikubwa cha upofu unaoweza kuzuilika.Kupitia kambi hii tumeweza kurejesha matumaini na tabasamu kwa wananchi wa Bagamoyo waliokuwa wakihitaji msaada wa kiafya,” amesema Dkt. Sharif.

More Stories
Dkt.Tulia,Mwalunenge waungana kutatua changamoto ya barabara
TUCASA yaomba kuanzishwa sheria malipo sekta ya ujenzi
Kihongosi:Uhai wa chama mashina